Jeshi la Kongo DR laua wanamgambo 36 wa Burundi
Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo limetangaza habari ya kuua wanachama 36 wa magenge mawili ya wanamgambo wa Burundi wanaobeba silaha, mashariki mwa nchi.
Msemaji wa jeshi la DRC, Dieudonne Kasereka amesema leo Ijumaa kuwa, wanachama hao wa magenge ya wanamgamo wa Burundi wameuawa katika operesheni ya siku tatu, iliyofanyika kati ya Aprili 6 na 8 huko mashariki mwa mkoa wa Kivu Kusini.
Ameongeza kuwa, wanajeshi watatu wa Kongo DR wameuawa pia katika makabiliano hayo ya kudhibiti maeneo yanayoshikiliwa na magenge ya wanamgambo ya National Liberation Forces (FNL) na Burundian Republican Forces (FOREBU).
Msemaji wa jeshi la DRC amebainisha kuwa, kamanda wa FNL, Jenerali Aloyse Zabampema amejeruhiwa vibaya katika operesheni hiyo. Amesisitiza kuwa, aghalabu ya maeneo yaliyokuwa chini ya magenge hayo ya wanamgambo kwa sasa yanadhibitiwa na jeshi la Kongo DR.
Ikumbukwe kuwa, Septemba 15 mwaka 2017, wakimbizi 15 wa Burundi walipigwa risasi na kuuawa na wanajeshi wa DRC wakishiriki maandamano katika mji wa Kamanyola mkoani Kivu ya Kusini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Mwito wa serikali ya Bujumbura wa kutaka kufanyika uchunguzi wa kina kuhusu mauaji hayo tatanishi uliangukia sikio la kufa.