Makumi ya raia wauawa kaskazini magharibi mwa Nigeria, jeshi latumwa kulinda amani
Serikali ya Nigeria imetangaza kuwa, raia wasiopungua 37 wameuawa katika mashambulizi yaliyofanywa na makundi ya watu wenye silaha huko kaskazini magharibi mwa Nigeria.
Taarifa iliyotolewa na serikali ya Nigeria imesema kuwa, Rais wa nchi hiyo Muhammadu Buhari amelaani mauaji ya raia 37 yaliyofanywa na makkundi ya watu wenye silaha katika jimbo la Sokoto kaskazini magharibi mwa nchi hiyo. Vyombo vya habari vinaripoti kuwa, mauaji hayo yalifanyika Ijumaa iliyopita.
Serikali ya Nigeria imetangaza kuwa imetuma jeshi katika eneo hilo kwa ajili ya kutuliza mambo na kulinda amani. Vilevile kikosi kingine cha jeshi na polisi kimepewa jukumu la kukabiliana na makundi ya wahalifu yaliyofanya mauaji na utekaji nyara wa watu mwaka uliopita.
Mwaka huu pekee makundi ya watu wenye silaha yameua mamia ya raia huko kaskazini magharibi mwa Nigeria na wengine wasiopungua elfu 20 wamelazimika kukimbia nyumba na makazi yao na kueleka nchi jirani na Niger.