Ripoti: Mabadiliko ya tabianchi yanakwamisha jitihada za kurejesha amani Somalia
Ripoti mpya ya Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Amani ya Stockholm (SIPRI) inaonyesha kuwa, mabadiliko ya tabianchi yamedumaza jitihada za sasa na za baadaye za kurejesha amani na utulivu nchini Somalia.
Uchunguzi wa taasisi hiyo ya kimataifa umebainisha kuwa, juhudi zinazofanywa za kurejesha amani, usalama na uthabiti nchini Somalia zinzofanywa na Ujumbe wa Umoja wa Mataifa katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika (UNSOM) zimeathiriwa na mabadiliko hayo ya hali ya hewa, sambamba na kuyapa nguvu makundi yenye misimamo ya kufurutu ada.
Kwa mujibu wa ripoti ya Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Amani ya Stockholm, mgogoro wa miongo kadhaa nchini Somalia umeshadidishwa na msururu wa ukame na baa la njaa, jambo ambalo limeiweka serikali katika mashinikizo na kufanya kuwa ngumu zaidi kazi na jitihada za Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo (UNSOM).
Florian Krampe, mtafiti wa ngazi za juu wa taasisi hiyo yenye makao makuu yake mjini Stockholm nchini Sweden anasema kuwa, ukame na mafuriko yameifanya idadi kubwa ya wananchi wa Somalia waachwe bila makao, na hivyo kuandaa mazingira kwa magenge ya kigaidi kama al-Shabaab kuwasajili wakimbizi hao wa ndani.
Takwimu za Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR zinaonesha kuwa, kuna wakimbizi wa ndani zaidi ya milioni 2.6 nchini Somalia, huku Wasomalia wengine wasiopungua laki nane wakiwa wakimbizi katika nchi jirani, kutokana na machafuko, migogoro na wimbi la ukame.