Wafuasi wa Sheikh Zakzaky waandamana Abuja wakitaka kuachiliwa huru kiongozi wao
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i62784-wafuasi_wa_sheikh_zakzaky_waandamana_abuja_wakitaka_kuachiliwa_huru_kiongozi_wao
Wafuasi wa Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria wameandamana katika mji mkuu Abuja wakilalamikia kuendelea kushikiliwa kizuizini kiongozi wao pamoja na mkewe.
(last modified 2026-02-05T09:20:29+00:00 )
Aug 13, 2020 03:41 UTC
  • Wafuasi wa Sheikh Zakzaky waandamana Abuja wakitaka kuachiliwa huru kiongozi wao

Wafuasi wa Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria wameandamana katika mji mkuu Abuja wakilalamikia kuendelea kushikiliwa kizuizini kiongozi wao pamoja na mkewe.

Waandamanaji hao wamejitokeza katika mitaa na barabara mbalimbali za mji mkuu Abuja wakiwa wamebeba mabango na maberamu pamoja na picha za Sheikh Zakzaky na kutoa wito wa kuachiliwa huru haraka kiongozi wao huyo tena bila masharti yoyote.

Muhammad Ibrahim Zakzaky mmoja wa watoto wa kiongozi huyo wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria ambaye hivi karibuni alifichua jinai zilizofanywa na serikali ya nchi hiyo dhidi ya familia yake na harakati hiyo amesema kuwa, serikali ya Rais Buhari imewaua watoto sita wa Sheikh Zakzaky.

Muhammad Ibrahim ameongeza kuwa, hali ya baba yake kiafya ni mbaya na imekuwa ikizidi kuwa mbaya siku baada ya siku.

Sheikh Ibrahim Zakzaky na mkewe Malama Zeenat walitiwa nguvuni tarehe 13 Desemba 2015 wakati wanajeshi wa Nigeria walipovamia Hussainia ya Baqiyatullah na nyumba ya mwanazuoni huyo katika mji wa Zaria. Waislamu wasiopungua 1,000, wakiwemo watoto watatu wa kiume wa Sheikh Zakzaky, waliuawa shahidi katika shambulio hilo.

Hatua kandamizi na za kikatili za polisi na jeshi la Nigeria dhidi ya wafuasi wa Sheikh Zakzaky zingali zinaendelea na hadi sasa idadi kubwa ya wafuasi wa kiongozi huyo wa kidini wamewekwa kizuizini au wameuawa shahidi.