Raisi: Israel italipa gharama ya kumuua mshauri wa kijeshi wa IRGC
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i106432-raisi_israel_italipa_gharama_ya_kumuua_mshauri_wa_kijeshi_wa_irgc
Rais wa Iran, Ebrahim Raisi, amesema utawala wa Kizayuni wa Israel utalipa gharama ya kitendo chake cha uhalifu cha kumuua mshauri mkuu wa kijeshi wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) nchini Syria.
(last modified 2026-02-21T22:51:18+00:00 )
Dec 25, 2023 23:53 UTC
  • Sayyid Ebrahim Raisi
    Sayyid Ebrahim Raisi

Rais wa Iran, Ebrahim Raisi, amesema utawala wa Kizayuni wa Israel utalipa gharama ya kitendo chake cha uhalifu cha kumuua mshauri mkuu wa kijeshi wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) nchini Syria.

Katika ujumbe wake uliotolewa jana Jumatatu, Sayyid Ebrahim Raisi alisema kitendo kiovu cha kumuua kigaidi mshauri wa jeshi la IRGC katika shambulio la makombora nchini Syria ni ishara nyingine ya kukata tamaa kwa utawala wa Kizayuni wa Israel.

Sayyid Razi Mousavi, ambaye alikuwa mshauri wa kijeshi nchini Syria, aliuawa katika shambulizi la anga la Israel katika kitongoji cha Sayyida Zainab katika mji mkuu wa Syria, Damascus mapema jana Jumatatu.

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu amesema, mshauri shupavu wa kijeshi ambaye alikuwa mmoja wa masahiba wa kamanda mkuu wa Iran wa kupambana na ugaidi, Luteni Jenerali Qassem Soleimani, ameuawa wakati "akilinda maadili aali ya Kiislamu."

Sayyid Razi Mousavi

Iran imetuma ujumbe wa washauri nchini Syria kwa ombi la serikali ya Damascus kwa lengo la kusaidia nchi hiyo ya Kiarabu iliyoharibiwa na vita kupambana na wanamgambo wanaoungwa mkono na mataifa ya kigeni ambao wamekuwa wakipigana na serikali ya Syria iliyochaguliwa kidemokrasia tangu 2011.

Wakati huo huo Waziri wa Mambo ya nchi za Nje wa Iran, Hossein Amir Abdollahian ametuma ujumbe wake wa rambirambi kwa mnasaba wa kuuawa shahidi kamanda Sayyid Razi Mousavi, mmoja wa washauri wakuu wa masuala ya kijeshi wa Iran nchini Syria akisisitiza kuwa, Tel Aviv inapaswa kusubiri siku ngumu.

"Tel Aviv isubiri siku ngumu sana", ameandika Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran katika ukurasa wake wa mtandao wa X.