Feb 01, 2024 12:25 UTC
  • Kuanza Alfajiri Kumi za Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran

Leo (Alhamisi), tarehe 12 Bahman 1402 Hijria Shamsia inayosadifiana na tarehe Mosi Februari 2024, ni mwanzo wa siku kumi zlizobarikiwa za alfajiri ya Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran.

Miaka 45 iliyopita katika siku kama hii ya leo, tarehe 12 mwezi Bahman mwaka 1357 Hijria Shamsia yaani ( Februari  Mosi mwaka 1979), Imam Ruhullah Khomeini, mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alirejea nchini baada ya kuishi uhamishoni kwa miaka kumi na tano na kulakiwa na mamilioni ya wananchi. Siku kumi baada ya kuwasili Iran, yaani tarehe 22 Bahman 1357 (Februari 11, 1979),Mapinduzi matukufu ya Kiislamu yalipata ushind kamili. Kwa sababu hiyo, kipindi cha kuanzia tarehe 12 Bahman, siku ambayo hayati Imam Khomeini aliwasili nchini Iran akitokea uhamishoni, hadi tarehe 22 Bahman, ambayo ni siku ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, kinaitwa "Alfajiri Kumi" na kila mwaka hufanyika sherehe maalumi za kuadhimisha ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu katika siku hizo.

Katika mkondo huo, jana (Jumatano), usiku wa kuamkia siku ya tarehe 12 Bahman, Ayatullah Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, kwa mujibu wa utaratibu wa miaka iliyopita, alizuru kaburi la Imam Khomeini (RA) na makaburi ya mashahidi wa harakati za kupigania Jamhuri ya Kiislamu na kuwakumbuka kwa kuwasomea Qur'ani na dua.

Ayatullah Khamenei akizuru kaburi la Imam Khomeini

Tarehe 12 Bahman ilikuwa hatua ya mabadiliko makubwa katika mapambano ya taifa la Iran dhidi ya utawala wa kifalme, na katika kipindii cha siku kumi baada ya Imam kuwasili nchini, mapinduzi ya taifa la Iran yalipata ushindi licha ya uungaji mkono na misaada ya Marekani na nchi nyingine za Magharibi kwa utawala wa Shah. Katika siku ya kwanza ya kurejea kwake nchini, Imam Khomeini alielekea moja kwa moja kwenye makaburi ya mashahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu eneo la Behesht Zahra, kwa ajili ya kutoa heshima kwa mashaujaa hao. Imam alitoa hotuba katika eneo hilo akisema kuwa, siri ya ushindi wa taifa la Iran ni umoja na mshikamano wa wananchi, na kuwa macho dhidi ya njama za maadui hususan shetani mkubwa, Marekani.

Sasa baada ya kupita miaka 45 tangu baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Marekani ingali inajaribu kuidhoofisha Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa kufanya njama za aina mbalimbali na kuwaunga mkono maadui zake. Hata hivyo wananchi wa Iran ambao wamevuka siku na vipindi vigumu kama vita vya kulazimishwa vya miaka 8 vilivyoanzishwa na dikteta wa zamani wa Iraq dhidi ya Iran, na sasa wanasonga mbele kwa umoja na mshikamano na kwa kufuata miongozo ya Kiongozi Muadhamu.

Katika kipindi chote hicho, taifa la Iran limeonyesha kwamba kamwe halitamruhusu adui kufikia malengo yake, na hii ndiyo sababu muhimu zaidi ya kuimarika Mapinduzi ya Kiislamu ambayo yanaendelea kusonga mbele kwa mafanikio katika nyanya za kikanda na kimataifa licha ya njama na vikwazo vyote vya Marekani na washirika wake.

Wachambuzi wengi wanakiri kwamba, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ndiyo mapinduzi muhimu na makubwa zaidi katika nusu ya pili ya karne ya 20, kwani wakati ulimwengu ulipokuwa umegawanyika kati ya madola mawili makubwa ya Mashariki na Magharibi, Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran yalipata ushindi chini ya uongozi wa Imam Khomeini kwa kauli mbiu ya "si Mashariki wala Magharibi" hapo tarehe 11 Februari 1979.

Eudo Steinbach, Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Mashariki ya Ujerumani anasema kuhusu umuhimu wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran na nafasi ya uongozi wa Imam Khomeini katika mapinduzi hayo kwamba: "Imam Khomeini alikuwa kiongozi wa kisiasa na kiroho mwenye haiba na mvuto mkubwa zaidi duniani; na malengo yote yaliyopatikana ya Jamhuri ya Kiislamu kwa mujibu wa misingi hiyo yametokana na fikra zake."

Imam Khomeini

Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, chini ya uongozi wa Imam Ruhuullah Khomeini na kisha Ayatullah Ali Khamenei, yamesababisha mabadiliko ya kimsingi katika nyanja mbalimbali za jamii ya Iran.

Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu Imam Khomeini, ambaye alikuwa na jukumu kubwa la kuliongoza taifa la Iran katika njia ngumu ya Mapinduzi ya Kiislamu hadi kufikia ushindi mkubwa tarehe 22 Bahman (11 Februari 1979), ni shakhsia asiye na kifani katika historia ya zama hizi ya Iran na amekuwa ushawishi mkubwa katika mwelekeo wa kisiasa na kihistoria na katika dunia ya sasa. Sasa baada ya kupita takriban miongo minne tangu kufariki dunia shakhsia huyo mkubwa katika historia ya Iran na ulimwengu wa Kiislamu, fikra na mitazamo yake bado inatambuliwa kuwa tochi iliyomulika njia Jamhuri ya Kiislamu.

Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ni miongoni mwa matukio muhimu na ya kipekee kabisa katika historia ya mwanadamu, ambayo yamekuwa na taathira kubwa katika nyanja mbalimbali za kiutamaduni, kisiasa, kijamii na kiuchumi ndani na nje ya Iran. Moja ya matunda ya mapinduzi hayo ni kuanzishwa Kambi ya Muqawama na harakati ya Umma mzima wa Kiislamu kwa ajili ya kukabiliana na ubeberu na Uzayuni, ambao matokeo yake tunayaona katika baadhi ya nchi kama Syria, Afghanistan, Yemen, Lebanon na Palestina.

Tags