Imamu Khamenei: Utawala wa Kizayuni umeshindwa kwa kutoweza kuuangamiza Muqawama
(last modified Wed, 23 Oct 2024 13:04:38 GMT )
Oct 23, 2024 13:04 UTC
  • Imamu Khamenei: Utawala wa Kizayuni umeshindwa kwa kutoweza kuuangamiza Muqawama

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, utawala wa Kizayuni umeshindwa katika njama yake ya kuuangamiza Muqawama licha ya kuua zaidi ya watu 50,000 wasio na hatia, lakini kushindwa kubaya zaidi ya huko ni fedheha na aibu uliyopata utamaduni, ustaarabu na wanasiasa wa Magharibi.

Mtandao wa Sahab umenukuu tovuti ya habari ya Ofisi ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu na kuripoti kuwa, katika kikao alichofanya na waandaaji wa Kongamano la Mashahidi 15,000 wa Mkoa wa Fars (kusini mwa Iran), Ayatullah Sayyid Khamenei amesema, matukio ya eneo, kusimama imara na Jihadi na Muqawama vimebadilisha hatima na historia ya eneo na akasisitiza kuwa, katika makabiliano kati ya kambi ya Muqawama na kambi ya uovu, ushindi utakuwa ni wa Muqawama.
 
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: kama wasingepatikana watu mithili ya Shahidi Sinwar wa kupambana hadi dakika ya mwisho, au kama wasingekuwepo shakhsia wakubwa kama Shahidi Sayyid Hassan Nasrullah wa kuchanganya pamoja Jihadi, hekima, ushujaa na kujitoa mhanga na kuvitumia hivyo katika medani, hatima ya eneo hili ingekuwa nyingine.
Imamu Khamenei akihutubia hadhara ya viongozi

Imamu Khamenei amesema: licha ya kuwaua shahidi zaidi ya watu 50,000 raia wasio na ulinzi na viongozi kadhaa mashuhuri wa Muqawama, na vilevile licha ya gharama kubwa ya fedha zilizotumika pamoja na uungaji mkono wa Marekani ambavyo vimewachafua na kuzusha chuki kubwa dhidi yao duniani, kambi ya Muqawama na vijana wanamapambano wa Hamas, Jihadul-Islami na Hizbullah pamoja na makundi mengine ya Muqawama wanapigana kwa nguvu na azma ileile, jambo ambalo ni pigo na kushindwa kukubwa kwa utawala wa Kizayuni.

 
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu ameendelea kueleza kwamba, kushindwa kukubwa zaidi ni kwa utamaduni na ustaarabu wa Magharibi; na akafafanua kwa kusema: kuwaua kwa halaiki watoto 10,000 wasio na hatia kwa mabomu ya tani mbili na silaha za kila aina, huku wanasiasa wa Magharibi wakionyesha kutoguswa hata chembe na hali hiyo, kumewafedhehesha wanasiasa hao warongo wa Magharibi na wanaojidai kuwa watetezi wa haki za binadamu, na hivyo kuuonyesha ulimwengu mzima kuwa ustaarabu wa Magharibi hauna thamani; na kwao wao, huko ni kushindwa kukubwa kabisa.
 
Ayatullah Khamenei ameitaja kambi inayouunga mkono utawala wa Kizayuni kuwa ni kambi ya uovu; na akaongeza kuwa: mkabala wa kambi hiyo ya uovu, imesimama kambi ya Muqawama; na kwa taufiki ya Mwenyezi Mungu, kambi hiyo ndiyo itakayopata ushindi.../