Kamanda: Jeshi la Iran litawaponda maadui wakifanya kosa lolote
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i124272-kamanda_jeshi_la_iran_litawaponda_maadui_wakifanya_kosa_lolote
Kamanda Mkuu wa Kikosi cha Nchi Kavu cha Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Brigedia Jenerali Kiumars Heidari amesema kikosi chake kiko macho na tayari kabisa kuwaangamiza maadui endapo watathubutu kufanya makosa yoyote dhidi ya taifa hili.
(last modified 2025-03-23T07:26:37+00:00 )
Mar 23, 2025 07:26 UTC
  • Kamanda: Jeshi la Iran litawaponda maadui wakifanya kosa lolote

Kamanda Mkuu wa Kikosi cha Nchi Kavu cha Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Brigedia Jenerali Kiumars Heidari amesema kikosi chake kiko macho na tayari kabisa kuwaangamiza maadui endapo watathubutu kufanya makosa yoyote dhidi ya taifa hili.

"Kikosi cha Ardhini cha Jeshi la Iran daima kiko macho, ange na tayari kusambaratisha maisha ya fedheha ya maadui iwapo kutatokea makosa yoyote," Heidari alisema hayo jana Jumamosi.

Brigedia Jenerali Heidari amebainisha kuwa, "Ni muhimu kwa vikosi vya kijeshi vya Iran daima kuimarisha utayarifu wao wa vita na uwezo wa kuzuia hujuma, ili kudhamini usalama endelevu wa Jamhuri ya Kiislamu."

Kamanda huyo mwandamizi wa Iran amebainisha, kuwa Vikosi vya Nchi Kavu vinajaribu kudumisha umakini wao kamili na kutegemea mafanikio ya hali ya juu ya ulinzi na usalama ili kudumisha usalama wa mpaka.

Matamshi ya Heidari yanakuja wakati huu Rais wa Marekani Donald Trump anaendelea kupiga ngoma ya vita dhidi ya Iran, huku akidai kuwa Tehran inaweza kukabiliwa kwa chaguo la kijeshi iwapo hakutafikiwa makubaliano kuhusu mpango wake wa nyuklia.

Kamanda Heidari ameeleza kuwa, "Kinachowatia kiwewe maadui wa Jamhuri ya Kiislamu hata zaidi ya silaha za kijeshi, ni taifa kubwa la Iran na uungaji mkono wake kwa mfumo."

Aidha Kamanda wa Kikosi cha Nchi Kavu cha Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuhusu uungaji mkono wa Iran kwa mataifa yanayodhulumiwa.