Amano: Iran imetekeleza mpango wa JCPOA
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) amesema kuwa Iran imetekeleza ahadi zake kuhusiana na Mpango Kamili ya Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA).
Yukia Amano amesema jana Jumatatu katika ripoti yake ya msimu kuhusu utekeleaji wa mpango wa JCPOA kuwa ripoti yake inathibitisha kusimamiwa shughuli za nyuklia za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kalibu ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa nambari 2231 la mwaka jana, na pia ni muhtasari wa uthibitisho wa usimamizi uliofanywa na Wakala wa IAEA katika miezi kadhaa iliyopita.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki Yukia Amano ameongeza kusema kuwa, wakala huo utaendelea kushirikiana na Iran. Kikao cha msimu cha Bodi ya Magavana ya wakala wa IAEA kilianza jana Jumatatu katika makao makuu ya wakala huo mjini Vienna Austria chini ya uwenyekiti wa Yukia Amano Mkurugenzi wa wakala huo kwa kujadili masuala mbalimbali ikiwemo Iran.
Ajenda kuu zitakazojadiliwa katika kikao hicho cha IAEA ni kuhusu kuchukuliwa hatua za lazima za kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kuboresha usafirishaji na usalama wa taka, mipango ya wakala huo kwa ajili ya kuimarisha usalama wa kinyuklia, kuboresha shughuli za wakala huo zinazohusiana na sayansi ya nyuklia, teknolojia na mipango mingine ya utekelezaji.