Saudia inaunga mkono wahalifu mashariki mwa Iran
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Iran Abdul Ridha Rahman Fadhli amesema Saudi Arabia inaunga mkono wahalifu katika eneo la mashariki mwa nchi.
Akizungumza Alhamisi katika mkoa wa Khorassan Razawi, Rahman Fadhli amesema Iran inakabiliwa na vitisho vya baadhi ya nchi za kigeni lakini haina wasiwasi kwani hatua imara zimechukuliwa kukabiliana na vitisho hivyo. Amesema hakuna shaka kuwa madola ya kibeberu yanataka machafuko yaibuke Iran na yamefanya kila yawezalo kufikia lengo hilo. Amesema Saudia imekuwa ikitoa misaada ya kifedha na kijasusi kwa wahalifu mashariki mwa Iran.
Kabla ya hapo pia, Kamanda wa Kikosi cha Nchi Kavu cha Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alifichua kuwa, baadhi ya madola katika eneo hasa Saudi Arabia imekuwa ikiunga mkono makundi ya kigaidi kwa lengo la kuvuruga amani ndani ya Iran. Brigedia Jenerali Ahmadreza Pourdastan aliongeza kuwa, Saudi Arabia ikiongozwa na Marekani na Utawala wa Kizayuni wa Israel imekuwa ikiunga mkono makundi ya kigaidi na kitakfiri ili yavuruge amani nchini.