Rais Rouhani awaasa Waislamu waungane dhidi ya njama za maadui
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i21490-rais_rouhani_awaasa_waislamu_waungane_dhidi_ya_njama_za_maadui
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amewataka Waislamu wote duniani waungane na kuimarisha umoja na mshikamano wao dhidi ya njama za maadui wanaotaka kuvunja umoja wa Waislamu kwa kuibua uhasama na mifarakano ya kimadhehebu.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Dec 15, 2016 11:05 UTC
  • Rais Rouhani awaasa Waislamu waungane dhidi ya njama za maadui

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amewataka Waislamu wote duniani waungane na kuimarisha umoja na mshikamano wao dhidi ya njama za maadui wanaotaka kuvunja umoja wa Waislamu kwa kuibua uhasama na mifarakano ya kimadhehebu.

Rais Rouhani ameyasema hayo katika Mkutano wa Kimataifa wa 30 wa Umoja wa Waislamu ulioanza leo mjini Tehran kwa kaulimbiu ya 'Udharura wa kupambana na makundi ya kitakfiri.'

Amesema umwagaji damu unaoendelea kushuhudiwa katika nchi za Kiislamu ni njama ya madola makubwa na utawala wa Kizayuni na kubainisha kuwa, lengo la maadui wa Uislamu, ni kuzima matumaini na fursa katika jamii za Waislamu duniani.

Mkutano wa Umoja wa Kiislamu waanza mjini Tehran

Kiongozi wa taifa wa Iran amesema Wamagharibi wakishirikiana na waitifaki wao katika eneo ndio wanaobeba dhima ya ubaharibifu katika miji ya Kiislamu kama vile Mosul sambamba na kukatwa vichwa vijana wa dini hiyo tukufu.

Rais Hassan Rouhani amesema ni jambo la kusikitisha namna baadhi ya nchi za Kiislamu zinavyoyapa fedha na silaha magenge ya kigaidi, huku akiwataka Maulamaa na wanafikra wa Kiislamu kuwaalika vijana katika ujumbe na mafundisho sahihi ya Uislamu, kwa kufuata mafundisho matukufu ya Mitume na haswa nyayo za Mtume Muhammad SAW.

Rais Rouhani amenukuu matamshi ya Imam Khomeini MA, aliyesema kuwa: "Mashia na Masunni ni mandugu, na kwamba kizingiti kinachosimama kati ya wafuasi wa madhehebu hizo mbili za Kiislamu, ni Uislamu wa Kimarekani."

Amesema anatumai kuwa Waislamu wataungana na kushikamana na mafundisho ya Qurani Tukufu na miongozo ya Mtume Muhammad SAW, sambamba na kutambua kuwa adui wao nambari moja ni utawala wa Kizayuni.

Baadhi ya viongozi wa Kiislamu wanaoshiriki mkutano wa Umoja wa Kiislamu

Mkutano huo ambao umefunguliwa rasmi na Rais Hassan Rouhani unahudhuriwa na maulama, wasomi na wanafikra wa Kiislamu zaidi ya 300 kutoka nchi mbalimbali za dunia na utaendelea kwa kipindi cha siku tatu.