Iran: Mapambano ya watu wanaopigania kujikomboa si ugaidi
Es'haq Al-e Habib, naibu wa mwakilishi wa kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa amesema katika kikao cha Baraza Kuu la umoja huo kuwa, mapambano ya wananchi wanaopigania kujikomboa kutoka katika makucha ya wavamizi wanaozikalia kwa mabavu ardhi zao, si ugaidi.
Shirika la habari la IRNA limemnukuu Es'haq Al-e Habib akisema hayo jana katika kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na huku akigusia nafasi ya kiistratijia na ya kimataifa ya umoja huo katika vita dhidi ya ugaidi amesema, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inapinga jaribio lolote la kuwaita magaidi watu wanaopigania kujikomboa au waliosimama kupambana na magaidi waliovamia nchi zao.
Amesema, wanachotarajia walimwengu ni kuuona Umoja wa Mataifa unatekeleza vizuri jukumu lake katika vita dhidi ya ugaidi bila ya kufanya undumakuwili wa aina yoyote na kwamba njia bora ya kupambana na ugaidi ni kutiwa nguvu ushirikiano uliosimama juu ya msingi wa uwazi na mshikamano.
Vile vile amesema, kwa kuzingatia hayo tutaona kuwa hatua yoyote ya upande mmoja ya kuandaa orodha ya nchi zinazodaiwa zinaunga mkono ugaidi, si hatua halali bali ni kitu kinachokinzana na starijia ya kupambana na ugaidi ya Umoja wa Mataifa.
Es'haq Al-e Habib pia amesema moja ya mapungufu yaliyomo katika starijia ya kupambana na ugaidi ya Umoja wa Mataifa ni kutozingatiwa muundo mkuu wa kupambana na ugaidi wa umoja huo.