Spika wa Bunge la Iran awasili Uturuki kushiriki mkutano wa Eurasia
Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran (Bunge) amewasili katika mji wa Antalya nchini Uturuki kwa ajili ya kushiriki katika Mkutano wa 3 wa Mabunge ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Eurasia.
Kabla ya kuelekea Uturuki, Ali Larijani alitaja lengo la kushiriki mkutano huo kuwa ni kujadili suala la ustawi wa nchi za eneo hilo na ubadilishanaji wa kibiashara kati ya nchi mbalimbali. Larijani ameongeza kuwa eneo la Eurasia ni miongoni mwa maeneo ambayo yanapaswa kupewa mazingatio.
Katika safari yake hiyo pia Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran atahutubia mkutano wa mabunge wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Eurasia, kufanya mazungumzo na Spika wa Bunge la Uturuki na baadhi ya maspika wa nchi zitakazoshiriki katika mkutano wa Antalya.
Maspika wa mabunge 20 na jumbe za maafisa wa bunge kutoka nchi 17 za Asia na Ulaya watahudhuria hafla ya ufunguzi wa mkutano hio itakayofanyika kesho Jumanne. Taarifa ya mwisho ya Mkutano wa Tatu wa Mabunge ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Eurasia itatolewa kesho Jumanne.