Majeshi ya Iran yako tayari kujenga hospitali mbili za muda Lebanon
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i62657-majeshi_ya_iran_yako_tayari_kujenga_hospitali_mbili_za_muda_lebanon
Mkuu wa Kamandi ya Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema, majeshi ya Iran yako tayari kujenga hospitali mbili za muda kwa ajili ya watu wa Lebanon iwapo serikali ya nchi hiyo itatoa ombi.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 06, 2020 21:54 UTC
  • Meja Jenerali Bagheri
    Meja Jenerali Bagheri

Mkuu wa Kamandi ya Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema, majeshi ya Iran yako tayari kujenga hospitali mbili za muda kwa ajili ya watu wa Lebanon iwapo serikali ya nchi hiyo itatoa ombi.

Meja Jenerali Bagheri, Mkuu wa Kamandi ya Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema Jeshi la Iran na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) yako tayari kujenga hospitali mbili za muda nchini Lebanon zitakazokuwa na vifaa na madaktari kutoka Iran. Huku akitoa salamu za rambi rambii kwa watu na serikali ya Lebanon kufuatia kupoteza maisha Walebanon katika mlipuko wa Bandari ya Beirut, Meja Jenerali Bagheri amesema Majeshi ya Iran yako tayari kuisaidia Lebanon katika nyanja zote.

Aidha amesema Iran itatoa msaada wowote unaohitajika kwa Lebanon wakati wa kujenga upya bandari ya Beirut.

Hali ilivyokuwa baada ya mlipuko wa Beirut

Tayari Hilali Nyekundu ya Iran imeshatuma shehena kubwa ya misaada kwa watu wa Lebanon sambamba na kujenga hospitali ya muda mjini Beirut kutoa huduma kwa waliojeruhiwa.

Moto uliozuka katika moja ya maghala ya  bandari ya Beirut Jumanne, ulienea na kusababisha mlipuko mkubwa katika maghala mengine ya jirani kulikokuwa kumewekwa Ammonium nitrate. Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Lebanon kufikia sasa kwa uchache watu 150 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 5000 kujeruhiwa katika mlipuko huo.