Naibu Kamanda wa SEPAH azionya Imarati na utawala haramu wa Israel
Naibu Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran SEPAH amezionya Imarati na utawala haramu wa Israel na kusisitiza kwamba, Iran itatoa jibu kali kwa chokochoko yoyote ile.
Jenerali Ali Fadavi amesema hayo katika mahojiano aliyofanyiwa na Shirika la Habari la Iran Press ambapo amesisisitiza kwamba, endapo Imarati na Israel zitafanya harakati japo ndogo yenye kutishia usalama wa taifa hili, basi Iran itatoa jibu kali kwa hatua hiyo.
Naibu Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran SEPAH ameongeza kuwa, uwanja huu mpya uliofunguliwa na Wazayuni na Wamarekani, utashindwa ilivyokuwa huko nyuma na ushindi utakuwa ni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Kamanda huyo mwandamizi wa Jeshi la Walinzi wa Mpainduzi ya Kiislamu SEPAH ameashiria pia njama za maadui za kutaka kutoa pigo dhidi ya Iran ya Kiislamu na kusema kuwa, uwezo na nguvu za Iran ni kubwa mno ikilinganishwa na miaka 41 iliyopita kiasi kwamba, zinamfanya adui asithubutu kuanzisha chokochoko dhidi ya taifa hili.
Kufuatia hatua kadhaa zilizochukuliwa na Rais Donald Trump wa Marekani kwa lengo la kurahisisha uanzishwaji wa uhusiano wa kawaida kati ya Imarati na utawala haramu wa Kizayuni, Alkhamisi iliyopita ya tarehe 13 Agosti pande mbili za Abu Dhabi na Tel Aviv zilisaini mkataba na kuafikiana rasmi kuanzisha uhusiano kamili wa kidiplomasia. Hatua hiyo imeendelea kulaaniwa na watu huru na wapigania uadilifu kote ulimwenguni.