Iran yaanza mazoezi makubwa ya kijeshi ya ulinzi wa anga
Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo yameanza mazoezi makubwa ya kijeshi yanayohusu ulinzi wa anga ambayo yanajumuisha Jeshi la Iran na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC)
Mazoezi hayo ya kijeshi ambayo yemepewa jina la 'Walinzi wa Anga ya Velayat-99' yanafanyika kwa lengo la kuinua kiwango cha utayarifu wa kivita na kuimarisha ushirikiano kioparesheni baina ya vikosi vyote husika vya ulinzi. Akizungumza na waandishi habari, msemaji wa mazoezi hayo, Brigedia Jenerali Qader Rahimzadeh amesema katika mazoezi hayo kutafanyika majaribio aina mbali mbali ya makombora na rada pamoja na mazoezi ya vita vya kieletrokini.
Ameongeza kuwa zana za kivita zitakazotumiwa katika mazoezi hayo zimeundwa na wataalamu wa ndani ya nchi.
Mazoezi hayo ambayo yatashabihiana na hali halisi ya kivita pia yatajumuisha ndege za kivita za Iran zikiwemo zile ambazo hazina rubani au drone.
Iran hufanya mazoezi makubwa ya kijeshi mara kwa mara ili kubaini uwezo na utayarifu wa vikosi vya ulinzi wa kujihami, na uwezo wake wa kijeshi si tishio kwa nchi yoyote bali sera zake za ulinzi zimejengeka katika msingi wa kujihami na kukabiliana na adui.