Qalibaf: Njama za maadui haziwezi kuzima Nuru ya Mtume Muhammad SAW
Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, Bunge la Iran, amesema nuru ya Mtume Mtukufu wa Uislamu, SAW, haiwezi kuzimwa kwa njama za maadui wa Kiislamu na kwamba njama hizo zitarejea kuwadhuru wao wenyewe.
Mohammad Baqer Qalibaf, Spika wa Bunge la Iran amesema waumini wameumizwa sana na uhasama wa wakuu wa Ufaransa kwa Mtume Muhammad SAW. Ameongeza, maadui ambao hawastahamili hata neno moja dhidi yao wamekithirisha chuki zao dhidi ya Uislamu.
Qalibaf amesema Bunge la Iran linalaani vikali hatua ya wakuu wa Ufaransa ya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW.
Akiashiria kauli ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Qalibaf amesema Mtume Muhammad SAW alitumwa kuleta umoja na ukarimu katika nyoyo za waja wa Mwenyezi Mungu.
Jarida la Kifaransa la Charlie Hebdo siku kadhaa zilizopita lilichapisha tena kibonzo kinachomtusi na kumvunjia heshima Mtume Muhammad (SAW).
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa alitetea kitendo hicho cha kutusiwa na kuvunjiwa heshima Mtume Muhammad SAW. Macron ambaye pia ametoa matamshi ya kuuvunjia heshima Uislamu amekosolewa vikali huku Waislamu duniani wakitoa wito wa kuiadhibu Paris kwa kususia bidhaa za Ufaransa.