Aug 12, 2023 03:56 UTC
  • Vita vya maneno baina ya Taliban na serikali ya Pakistan vingali vinaendelea

Waziri wa Mambo ya Nje wa Pakistan amelihutubu kundi la Taliban linalotawala nchini Afghanistan akisema: "amani na usalama wa Pakistan haviwezi kufanyiwa mchezo".

Kwa mujibu wa shirika la habari la Tasnim, Bilawal Bhutto Zardari, amesisitiza ulazima wa kuwa na maelewano na Kabul sambamba na kueleza bayana kuwa amani na usalama wa Pakistan haviwezi kufanyiwa mchezo.

Zardari, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Watu wa Pakistan amebainisha pia hamu ya nchi yake ya kuwa na maelewano ya dhati na ya ujengaji, kikanda na kimataifa kwa lengo la kuimarisha amani, usalama na utulivu nchini Afghanistan.

Ikumbukwe kuwa hivi karibuni msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid, alikanusha tuhuma zilizotolewa na Islamabad dhidi ya serikali ya kundi hilo. Sambamba na kupinga ufanyaji mashambulizi ya kigaidi ndani ya Pakistan, Mujahid alirudia na kutilia mkazo ahadi ya kundi hilo kwa kusema, "serikali ya mpito ya Taliban haitaruhusu mtu au kikundi chochote kutumia ardhi ya Afghanistan dhidi ya Pakistan, lakini Kabul haina masuulia ya kuzuia mashambulizi yanayofanywa ndani ya ardhi ya Pakistan na badala ya kuzusha tuhuma, viongozi wa Pakistan inawapasa wafanye juhudi za kuimarisha usalama wa nchi hiyo".

Bilawal Bhutto Zardari

Hadi kitambo si kirefu nyuma, Pakistan ilikuwa ikijulikana kama muungaji mkono wa Taliban. Lakini katika miezi ya karibuni, uhusiano kati ya nchi hiyo na Afghanistan iliyo chini ya utawala wa Taliban umetawaliwa na mikwaruzano na mivutano.

 
Kundi la Tehreek-e-Taliban la Pakistan linatajwa na serikali ya Islamabad kama tishio kuu la kigaidi nchini humo, na wanavyoamini maafisa wa Pakistan, kundi hilo linatekeleza hujuma zake za kigaidi kutokea  ardhi ya Afghanistan. Licha ya dhana hiyo kukanushwa na Taliban, uhusiano kati ya Islamabad na kundi hilo umeharibika kutokana na tuhuma hizo.
 
Kwa mujibu wa baadhi ya maafisa wa ngazi za juu wa Taliban, wanachama wa kundi hilo wanataka waruhusiwe wakapigane vita na Pakistan na kwamba miito ya ombi hilo imeongezeka kiasi kwamba inasemekana kiongozi wa Taliban Hebatullah Akhundzada hivi karibuni alitoa fatwa mpya isemayo, haijuzu kwenda kupigana vita Pakistan.../

Tags