Apr 25, 2024 07:32 UTC
  • Afrika Kusini yataka uchunguzi wa haraka kuhusu makaburi ya halaiki Ukanda wa Gaza

Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Afrika Kusini imetoa mwito wa kufanyika uchunguzi wa haraka na wa kina kuhusu makaburi ya umati yaliyogunduliwa katika Ukanda wa Gaza.

Kwa mujibu wa Kanali ya Televisheni ya Al-Mayadeen, Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Afrika Kusini imetoa mwito huo katika taarifa yake leo na kubainisha kuwa, utawala wa Kizayuni umepuuza hukumu za Mahakama ya Kimataifa ya Uadilifu katika vita dhidi ya Ukanda wa Gaza, na hadi sasa hakuna adhabu iliyotolewa kwa utawala huu na hivyo kutaka kufanyika uchunguzi wa haraka na wa kina juu ya makaburi ya umati yaliyogunduliwa katika ukanda wa Gaza.

Juzi wafanyakazi wa utumishi wa umma huko Gaza waliopoa miili ya Wapalestina 283 katika makaburi kadhaa ya umati katika yadi ya Hospitali ya Nasser huko Khan Yunis, wengi wao wakiwa wanawake, watoto na wazee. Baadhi ya waliouawa walikuwa wamefungwa macho na kufungwa pingu.

Hayo yanajiri katika hali ambayo, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa ametoa wito wa kufanyika uchunguzi wa kimataifa kuhusu makaburi ya umati yaliyogunduliwa katika hospitali kuu mbili za Ukanda wa Gaza.

 

Wito huo wa Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa unafuatia ule uliotolewa Stefan Dujarric, msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ambaye ametaka kufanyike uchunguzi wa kuaminika, kamili na huru kuhusu makaburi ya halaiki yaliyogunduliwa katika Hospitali ya Nasser huko Khan Yunis, kusini mwa Ukanda wa Gaza, baada ya wamajeshi wa Israel kuondoka katika eneo hilo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, Volker Turk, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa ametoa wito wa kufanyika uchunguzi wa kimataifa kuhusu makaburi ya umati yaliyogunduliwa katika hospitali kuu mbili za Ukanda wa Gaza, na kusema kwamba ameshtushwa sana na uharibifu uliofanyika katika wa Hospitali ya Al-Shafa na kituo cha Matibabu cha Nasser.