Askofu Mkuu wa Canterbury asema lazima Israel ikomeshe vita Gaza
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i104780-askofu_mkuu_wa_canterbury_asema_lazima_israel_ikomeshe_vita_gaza
Askofu Mkuu wa Canterbury amesema hakuna msingi wowote wa kimaadili unaoweza kuhalalisha mauaji ya Wapalestina huko Gaza ambayo yanatekelezwa na utawala wa Israel.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 15, 2023 00:25 UTC
  • Askofu Mkuu wa Canterbury asema lazima Israel ikomeshe vita Gaza

Askofu Mkuu wa Canterbury amesema hakuna msingi wowote wa kimaadili unaoweza kuhalalisha mauaji ya Wapalestina huko Gaza ambayo yanatekelezwa na utawala wa Israel.

Vifo vya raia na "janga la kibinadamu" kutokana na mashambulizi ya Israel na kuzingirwa kwa Ukanda wa Gaza haviwezi kuhalalishwa kimaadili, Justin Welby alisema.

"Umwagaji damu lazima ukome", alisema katika Sinodi Kuu ya Kanisa la Uingereza siku ya Jumatatu. Hakuna uhalali wa kimaadili kwa "hasara mbaya ya maisha ya raia" huko Gaza, aliongeza.

Askofu huyo aliongeza kuwa: "... Nataka kuweka wazi kwamba siamini kwamba hasara kubwa ya maisha ya raia na maafa ya kibinadamu yanayotokana na mashambulizi ya Israel na kuzingirwa kwa Gaza yanaweza kuwa ya haki."

Alisema, tangu wito wa "kusitishwa mara moja kwa mapigano ya kibinadamu" kutoka kwake na viongozi wengine wa Kikristo wakati wa ziara ya al-Quds (Jerusalem) zaidi ya wiki tatu zilizopita, "maelfu zaidi ya wanaume, wanawake na watoto wasio na hatia huko Gaza wameuawa."

"Kwa hiyo narudia wito huo tena kwa uharaka mpya na nguvu zaidi: umwagaji damu huu lazima ukome, mateka lazima waachiliwe na misaada lazima iwafikie wale walio katika Gaza wenye uhitaji mkubwa," Askofu Mkuu alisema.