Lebanon yatangaza baraza jipya la mawaziri linaoongozwa na Hariri
Lebanon imetangaza baraza jipya la mawaziri linaloongozwa na Waziri Mkuu, Saad al-Hariri, wiki 6 baada ya kuchaguliwa Rais Michel Aoun.
Televisheni ya serikali iliyatangaza hayo jana Jumapili na kuongeza kuwa, baraza hilo litakuwa na mawaziri 30. Baadhi ya walioteuliwa kushika nyadhifa hizo ni Gebran Bassil, Waziri wa Mambo ya Nje, Ali Hassan Khalil, Waziri wa Fedha, Nouhad Machnouk, Waziri wa Mambo ya Ndani huku Wizara ya Ulinzi ikipewa Yacoub al-Sarraf.
Saad al-Hariri, Waziri Mkuu wa Lebanon amesema serikali hiyo imejumuisha watu wa jamii na matabaka yote ya nchi, licha ya chama cha Kikristo cha Phalangist kususia wizara iliyotengewa.
Mapema mwezi uliopita, Rais Michel Aoun wa Lebanon ambaye ni muitifaki wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah, alimteua Hariri, kiongozi wa harakati ya al-Musatqbal kuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo.
Kwa mujibu wa Katiba ya Lebanon, Rais wa nchi anapasa kutoka miongoni mwa Wakristo wa Maroni, Waziri Mkuu jamii ya Waislamu wa Kisunni na Spika wa Bunge awe anatoka jamii ya Waislamu wa Kishia.
Baada ya kupita zaidi ya miaka miwili ya mkwamo wa kisiasa, Oktoba 31, Bunge la Lebanon lilifanya kikao chake cha 46 cha upigaji kura na hatimaye kumchagua Michel Aoun mwenye umri wa miaka 81 kuwa rais mpya wa nchi hiyo.