Saudia yalaani sheria ya JASTA ya Marekani
Ubalozi wa Saudia mjini Washington Marekani umelaani sheria iliyo dhidi ya wafadhili wa ugaidi kwa kifupi JASTA ya nchini Marekani.
Katika ujumbe wake mfupi kupitia mtandao wa kijamii wa Tweeter, ubalozi wa Saudi Arabia mjini Washington sambamba na kulaani sheria hiyo umedai kuwa, italeta vikwazo vingi kwa mamlaka za kijeshi za nchi hizo mbili.
Ikumbukwe kuwa, Baraza la Sanate la Marekani limepiga kura ya kubatilisha veto ya Rais Barack Obama wa nchi hiyo aliyepinga kufuatiliwa wahusika wa mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11 nchini Marekani ambapo mashtaka hayo yaliwahusisha moja kwa moja viongozi wa Saudia kwenye mashambulizi hayo. Baraza la Sanate la Marekani limetengua veto ya Obama kwa kura 97 za ndio na moja tu ya hapana.
Viongozi wa Saudi Arabia wanadai kuwa, sheria ya JASTA inadharau msingi wa kujitawala nchi nyingine na kwamba sambamba na kuwa na madhara makubwa ya kiuchumi, itakuwa na madhara pia ya kisiasa iwapo itatekelezwa.
Kwa mujibu wa sheria hiyo ya JASTA, familia za wahanga wa mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11, 2001 nchini Marekani wana haki ya kuomba fidia kutoka kwa Saudi Arabia, kwani watu 15 kati ya 19 walioteka ndege zilizotumika kwenye mashambulizi ya Septemba 11 nchini Marekani, walikuwa raia wa Saudi Arabia.