Ndege za Marekani zaua raia wengine 11 Raqqah, Syria
Raia 11 wasio na hatia wamepoteza maisha baada ya ndege za muungano vamizi wa kimataifa unaodai kupambana na Daesh na ambao unaongozwa na Marekani kufanya mashambulizi huko Raqqah, nchini Syria.
Miongoni mwa wahanga wa jinai hiyo, ni watoto wadogo watano ambapo kwa mujibu wa mashuhuda, raia wawili wameuawa katika shambulizi dhidi ya kijiji cha Ghadhban huku wengine tisa wakiwamo watoto hao watano wakiuawa katika kijiji cha Suwaidah.
Habari Zaidi zimeeleza kuwa, hujuma hizo zimejeruhi watu wengi na hali ya baadhi yao nii mahututi. Siku chache zilizopita, ndege za muungano huo vamizi zilifanya shambulizi kama hilo katika eneo la al‑Mushairifa ndani ya mji huo wa Raqqah na kuua kikatili raia wasiopungua 28 na kujeruhi makumi ya wengine.
Kabla ya hapo ndege za muungano huo unaoongozwa na Marekani, zilifanya hujuma nyingine katika kijiji cha al-Haishat na kuua raia 23 akiwemo mtoto mmoja mdogo.
Inafaa kuashiria kwamba, mashambulizi ya ndege hizo za Marekani na waitifaki wake nchini Syria, yanafanywa bila ya idhini ya serikali ya Damascus kwa madai ya kile kinachotajwa na Washington kwamba eti ni mapambano dhidi ya genge la Daesh (ISIS). Ushahidi unaonyesha kwamba, tangu muungano huo ulipoanza operesheni hizo bandia, umekuwa ukihusika mno kuua raia wa kawaida na askari wa serikali ya Syria, badala ya kuwalenga magaidi.