Yemen yakosoa kimya cha jamii ya kimataifa kuhusu jinai za Saudia
Waziri wa Mambo ya Nje wa Serikali ya Uokovu wa Kitaifa ya Yemen ameikosoa jamii ya kimataifa kwa kushindwa kusimamisha jinai, vita na mzingiro uliowekwa dhidi ya nchi hiyo.
Hisham Sharaf Abdullah ameashiria kikao cha pande nne kilichofanyika jana Jumatatu huko Amman Jordan kikihudhuriwa na Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Yemen na kueleza kuwa, Marekani, Uingereza, Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) zinawashambulia watu wa Yemen na kwamba hakuna mashinikizo yoyote kutoka jamii ya kimataifa kwa lengo la kusimamisha vita na kuhitimisha mzingiro dhidi ya nchi ya Yemen.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Yemen amesisitiza kuwa Saudia ndiyo iliyoanzisha vita dhidi ya wananchi madhlumu wa Yemen na inayaunga mkono na kuyasaidia kifedha makundi yenye silaha ya huko Yemen.
Hisham Sharaf Abdullah ameongeza kuwa, Saudi Arabia imeitumbukiza Yemen katika hali ya mchafukoge mbali na kuyapatia silaha, fedha na suhula za kiistratejia makundi ya waasi.