Kiongozi wa Ansarullah: Saudia, UAE zatekeleza njama za ubeberu wa Marekani
Kiongozi wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen amesema tawala za Saudia na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) zinaongoza katika kutekeleza njama za ubeberu katika eneo la Mashariki ya Kati.
Abdul Malik al Houthi, Kiongozi wa Ansarullah ameyasema hayo Jumamosi akiwahutubia waumini waliokusanyika nchini humo katika maombolezo ya kuuawa shahidi Imam Hussein AS. Katika hotuba yake amewapongeza wananchi wa Yemen kwa kusimama kidete kukabiliana na wavamizi wa kigeni wanaoongozwa na Saudia. Aidha ametoa wito kwa Wayemen kudumisha umoja na mashikamano wao ili wawezek kukabiliana na maadui.
Kiongozi wa harakati ya Ansarullah halikadhalika ametangaza kuunga mkono harakati za mapambano na muqawama huko Palestina na Lebanon huku akisisitiza kukabiliana na njama za Marekani na uistikabri wa kimataifa nchini Yemen.
Al Houthi amesema kuibuka misiguano baina ya vikosi mbali mbali vya Yemen ni jambo lililo kinyume cha maslahi ya kitaifa na ni kwa manufaa ya Marekani, Israel, Saudia na Imarati.
Kiongozi wa Ansarullah aidha amesema, falsfa ya Ashura na maombolezo ya Imam Hussein AS ni kuwa, Mapinduzi ya Imam Hussein AS ni ya kudumu na vizazi vyote vitaendelea kunufaika na mapinduzi hayo.