Umoja wa Ulaya walalamikia jinai za Israel
Umoja wa Ulaya umeutaka utawala ghasibu wa Kizayuni ukomeshe kuvunja nyumba za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Umoja huo umetoa tamko na kusema kuwa ofisi zake katika miji ya Baytul Muqaddas na Ramallah huko Palestina zimeanza kufuatilia uharibifu na uporaji unaofanywa na Israel dhidi ya nyumba za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. Mwito huo wa Umoja wa Ulaya umetolewa katika hali ambayo jeshi la Israel hivi karibuni lilitoa amri ya kuvunjwa nyumba za Wapalestina katika maeneo ya 'Ayn al Halwah na Ummul Jamal katika bonde la Jordan, katika Ukingo wa Magharibi.
Umoja wa Ulaya aidha umelaani lengo la Israel la kuvunja nyumba 20 za kijiji cha Suwaisiyyah (?) cha Wapalestina na kusema kuwa, iwapo utawala wa Kizayuni utavunja nyumba za kijiji hicho wakati huu wa baridi kali basi wakazi mia moja wa kijiji hicho nusu yao wakiwa ni watoto wadogo, watashindwa na pa kukimbilia. Wiki iliyopita utawala wa Kizayuni ulitoa amri kama hiyo kuhusu eneo la jabal al Bab nje ya kitongoji kimoja cha walowezi wa Kizayuni karibu na mji mtakatifu wa Baytul Muqaddas.
Uporaji wa ardhi za Wapalestina na kujenga vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi hizo za Wapalestina ndiyo mbinu kubwa inayotumiwa na utawala dhalimu wa Kizayuni kwa ajili ya kuvuruga muundo wa kijamii wa Palestina. Utawala huo pandikizi unadharau sheria zote za kimataifa, hata azimio nambari 2334 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linalolaani ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi wanazoporwa Wapalestina.