Ansarullah ya Yemen yaionya Saudi Arabia
Katibu Mkuu wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen ameutahadharisha utawala wa Aal Saud na kutangaza kwamba, katika siku chache zijazo Saudia itashtukizwa na harakati hiyo.
Abdul-Malik Badreddin al-Houthi ameandika katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter akiwahutubu viongozi wa Saudia kwamba: Kama ambavyo katika siku za nyuma tuliahidi tutashambulia kwa kombora eneo walipo mamluki vamizi wa Aal Saud huko Taiz, muda si mrefu pia mtafahamu kuwa, hatujasahau suala la kuwalipizia kisasi.
Juzi Jumatatu, vikosi vya Yemen vilifyatua kombora la balestiki na kuangamiza makumi ya mamluki wa Saudi Arabia katika mkoa wa Taizz, kusini mashariki mwa nchi.
Vikosi vya Yemen vilifyatua kombora hilo aina ya Qaher 2-M kuelekea katika kambi ya mamluki hao mjini al Khayami katika mkoa wa Taiz.
Tangu mwezi Machi mwaka 2015, Saudia, ikisaidiwa na kuungwa mkono na baadhi ya nchi za Kiarabu na Marekani ilianzisha mashambulio ya kinyama dhidi ya Yemen kwa lengo la kutaka kumrejesha madarakani kibaraka wake Abd Rabbuh Mansur Hadi, rais wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kuitoroka nchi.
Raia zaidi ya elfu 13 wa Yemen wameuawa, hasa wanawake na watoto, na maelfu ya wengine kujeruhiwa katika uvamizi huo wa kijeshi huku Umoja wa Mataifa ukishindwa kuchukua hatua yoyote ya kuzuia jinai hizo za Saudia huko Yemen.