Iraq yamtimua mwanadiplomasia wa Saudia
Serikali ya Iraq imemtimua mwanadiplomasia mmoja wa Saudia kwa tuhuma za kuingilia uchaguzi wa bunge uliopita nchini humo.
Duru za habari nchini Iraq zimetangaza kwamba serikali ya Baghdad imemtimua Yahya Sharahili ambaye pia alikuwa msaidizi wa zamani wa balozi wa Saudia mjini Baghdad. Kabla ya uchaguzi wa bunge uliopita, Sharahili ambaye awali aliondoka nchini Iraq mwaka 2016 na amekuwa akihudumu kama Naibu wa Thamer Al-Sabhan, Waziri Mshauri wa Saudia katika masuala ya eneo la Ghuba ya Uajemi, aliwasiliana na pande tofauti za kisiasa, Kishia na Kisuni nchini Iraq ili kuathiri matokeo ya uchaguzi huo.
Miaka miwili iliyopita, Thamer Al-Sabhan, balozi wa zamani wa Saudia nchini Iraq alitimuliwa na serikali ya Baghdad kwa tuhuma za kufanya mawasiliano na uungaji mkono kwa kundi la kigaidi la Daesh (ISIS). Uchaguzi wa bunge nchini Iraq ulifanyika tarehe 12 Mei mwaka huu kwa kuwashirikisha Wairaq milioni 11 ambapo kiwango cha ushiriki kilifikia asilimia 44.