HRW: Israel inafanya jinai za kivita huko Gaza
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limetangaza kuwa utawala wa Kizayuni wa Israel unafanya jinai za kivita dhidi ya raia wanaoandamana huko katika Ukanda wa Gaza, Palestina.
Ripoti iliyotolewa leo na Human Rights Watch imesema kuwa, mauaji yanayofanywa mara kwa mara na askari wa utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya waandamanaji huko katika Ukanda wa Gaza ni jinai za kivita.
Ripoti hiyo imesema kuwa, utumiaji wa nguvu na zana za mauaji bila ya kuwepo tishio lolote linalowakabili Waisraeli, unapelekea kuuawa na kujeruhiwa idadi kubwa ya raia wa Palestina.
Human Rights Watch imesisitiza kuwa, jamii ya kimataifa inapaswa kukomesha hali hiyo na kwamba Israel imekuwa ikitoa ripoti za mara kwa mara kuihalalisha, huku Marekani ikitumia kura ya veto kuzuia hatua zote za kuuadhibu utawala huo.
Ripoti ya Human Rights Watch inasema kuwa, Kuwait imewasilisha pendekezo la kulaaniwa Israel katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa sababu ya kutumia risasi za vita dhidi ya raia wa Palestina katika Ukanda wa Gaza.