Intifadha yazidi kuutia kiwewe utawala wa Kizayuni wa Israel
Majenerali wa kijeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wamesema kuwa, wana wasiwasi wa kuongezeka muqawama wa wananchi wa Palestina dhidi ya utawala huo pandikizi.
Shirika la habari la Palestina SAMA limemnukuu kamanda wa taarifa za kijasusi wa jeshi la utawala wa Kizayuni akisema kuwa, hali katika ardhi za Palestina inazidi kuwa mbaya huku upinzani dhidi ya utawala wa Kizayuni ukizidi kuwa mkubwa hususan katika vitongoji vya walowezi wa Kizayuni vilivyoko katika maeneo yaliyobakia ya Wapalestina. Afisa huyo mwandamizi wa masuala ya kijasusi katika jeshi la Israel ambaye pia ni mjumbe katika kamati ya siasa za kigeni za bunge la utawala wa Kizayuni KNESET ameongeza kuwa, kuzorota ujenzi mpya wa Ukanda wa Ghaza baada ya vita vya mwaka 2014 kunaongeza hasira za Wapalestina na kuwafanya wawe tayari kuchukua hatua yoyote ile kulipiza kisasi cha mashambulizi hayo ya Israel katika ukanda huo. Kamanda huyo wa taarifa za kijasusi wa jeshi la utawala wa Kizayuni ameongeza kuwa, iwapo hali ya kiuchumi itaboreka huko Ghaza, huenda jambo hilo likapunguza hasira za Wapalestina wakiwemo wale wa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. Katika miezi ya hivi karibuni, walowezi wa Kizayuni na wanajeshi wa Israel wameongeza jinai zao dhidi ya Wapalestina kiasi kwamba wamepelekea mamia ya Wapalestina kuuawa shahidi na kujeruhiwa, suala ambalo limezidi kuwakasirisha Wapalestina.