Magaidi 5 wa Daesh watiwa mbaroni katika mkoa wa Salahuddin Iraq
Askari jeshi wa Iraq wamewatia mbarono magaidi watano wa kundi la kitakfiri la Daesh katika oparesheni waliyoifanya katika mkoa wa Salahuddin nchini humo.
Jeshi la Iraq leo Jumanne limeshambulia ngome za magaidi wa Daesh katika eneo moja mkoani Salahuddin na kufanikiwa kuwatia mbaroni magaidi hao. Wanajeshi wa Iraq wamemtia mbaroni pia gaidi mwingine wa Daesh katika mkoa wa Kirkuk kaskazini mwa nchi hiyo aliyekuwa akisakwa.
Wakati huo huo chombo kimoja cha usalama kimeripoti juu ya kugunduliwa kaburi moja la umati la wahanga wa mashambulizi ya kundi la kigaidi la Daesh huko katika kijiji cha Daoud al Aluka katika mkoa wa Kirkuk.
Aidha miili ya watu 45 wa kijiji hicho imetambuliwa kwenye kaburi hilo la umati ambao waliuawa na mamluki wa Daesh wakati walipokuwa wakilidhibiti eneo hilo.
Masalia ya magaidi wa Daesh bado yapo katika maeneo mbalimbali ya Iraq licha ya kundi hilo kupata pigo na kufurushwa nchini humo. Jeshi la Iraq na kundi la wapinagaji wa al Hashdu al Shaa'bi wanaendelea kutekeleza oparesheni mbalimbali za kuwaangamiza masalia ya magaidi wa Daesh nchini humo.