Kukimbia mateka wa Kipalestina, pigo kwa usalama wa utawala wa Kizayuni
Waziri wa Usalama wa Ndani wa utawala wa Kizayuni wa Israel amekiri kuwa kukimbia mateka 6 wa Kipalestina ni pigo kubwa kwa usalama wa utawala huo.
Omer Barlev jana alitembelea gereza la Ktzi'ot lililoko katika eneo la jangwani la Negeb kusini mwa Palestina inayokaliwa kwa mabavu na kueleza kuwa, viongozi wa utawala huo wanawasaka mateka sita wa Kipalestina waliokimbia gereza hilo.
Barlev amesisitiza udharura wa kufanyika uchunguzi haraka iwezekanavyo na wa pande zote kujua namna mateka hao wa Kipalestina walivyokimbia. Amesema, walinzi na askari usalama kadhaa wa jela yenye ulinzi mkali ya Gilboa hivi sasa wametiwa nguvuni na wanaendelea kuhojiwa.
Waziri wa Usalama wa Ndani wa utawala wa Kizayuni wa Israel amesema kuwa, katika uchunguzi wa awali kuhusu namna mateka sita wa Kipalestina walivyotoroka jela hilo imebainika kuwa kamera zilizofungwa ndani ya gereza zilishindwa kuchukua picha wakati mateka hao walipotoroka, hata hivyo nukta ya kuzingatia ni kuwa, maafisa husika waliokuwepo katika chumba cha kudhibiti kamera walikuwa wamesinzia wakati wa kujiri tukio hilo.
Alfajiri ya Jumatatu wiki hii mateka watano wa Kipalestina wanachama wa harakati ya Jihad Islami na mmoja na harakati ya Fat-h ambao walihukumiwa kifungo cha muda mrefu walifanikiwa kutoroka jela ya Gilboa yenye ulinzi mkali huko kaskazini mwa Palestina inayokaliwa kwa mabavu ambayo ni moja kati ya jela kuu za kiusalama za utawala haramu za Israel.
