Mtafiti wa Kizayuni: Israel inamomonyoka ndani kwa ndani
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i93512-mtafiti_wa_kizayuni_israel_inamomonyoka_ndani_kwa_ndani
Mtafiti wa Kizayuni Profesa Daniel Kahneman amekosoa hatua za baraza la mawaziri la mrengo wa kulia wenye misimamo ya kufurutu mpaka linaloongozwa na waziri mkuu wa utawala haramu wa Israel Benjamin Netanyahu hususan kuhusiana na mageuzi ya Idara ya mahakama na kusema kuwa, hatua hizo zinamaanisha kumomonyoka ndani kwa ndani na kumalizika utawala wa Kizayuni.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jan 31, 2023 08:04 UTC
  • Mtafiti wa Kizayuni: Israel inamomonyoka ndani kwa ndani

Mtafiti wa Kizayuni Profesa Daniel Kahneman amekosoa hatua za baraza la mawaziri la mrengo wa kulia wenye misimamo ya kufurutu mpaka linaloongozwa na waziri mkuu wa utawala haramu wa Israel Benjamin Netanyahu hususan kuhusiana na mageuzi ya Idara ya mahakama na kusema kuwa, hatua hizo zinamaanisha kumomonyoka ndani kwa ndani na kumalizika utawala wa Kizayuni.

Maelfu ya Wazayuni katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina zilizopewa jina la Israel, wamekuwa wakiandamana kwa wiki kadhaa sasa, huku kila Jumamosi usiku wakifanya hivyo huko Tel Aviv na katika miji mingine kadhaa ya ardhi zinazokaliwa kwa mabavu wakipinga kile walichokiita "mapinduzi ya kisiasa" na kulalamikia maamuzi na sera za baraza la mawaziri lenye misimamo ya kufurutu ada linaloongozwa na Netanyahu
Vyombo vya habari vya Kizayuni vimekadiria idadi ya waandamanaji kuwa makumi ya maelfu.
Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Profesa Daniel Kahneman, mtafiti wa Kizayuni aliyeshinda Tuzo ya Nobeli ya Uchumi mwaka 2002, ameeleza katika mahojiano na chaneli ya 12 ya utawala wa Kizayuni kwamba, hivi sasa ana wasiwasi zaidi na hali ya utawala huo kuliko alivyokuwa wakati wa vita vya Oktoba 1973. 
Maandamano ya wazayuni wa kupinga sera za Netanyahu

Akiashiria mpango wa baraza la mawaziri lenye misimamo ya kufurutu mpaka la Netanyahu wa kutekeleza mageuzi katika mfumo wa mahakama, ambayo yamesababisha maandamano makubwa ya upinzani katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu, Kahneman amesema, "kinachonitia wasiwasi zaidi ni mapinduzi ya idara ya mahakama".

Mtafiti huyo wa Kizayuni ameongezea kwa kusema, "kwa maoni yangu, huu ni mwisho wa dunia na mwisho wa Israel niliyokuwa nikiijua mimi". Kahneman amefafanua kwa kusema, "nikilinganisha kiwango cha wasiwasi wangu juu ya Israel nimebaini kuwa, wasiwasi nilionao sasa ni mkubwa zaidi kuliko wakati wa vita vya Oktoba 1973 (vita kati ya Waarabu na utawala wa Kizayuni). Wakati ule sikuwa na wasiwasi kiasi hiki, ilhali sasa hivi nina wasiwasi juu ya dhati ya Israel yenyewe".../