AI: Lazima utawala wa Israel uvunje mfumo wa ubaguzi wa rangi
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i93600-ai_lazima_utawala_wa_israel_uvunje_mfumo_wa_ubaguzi_wa_rangi
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limesema utawala wa Israel "lazima uvunje mfumo wa ubaguzi wa rangi au apathaidi ambao unasababisha mateso na umwagaji damu mkubwa" katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.
(last modified 2026-07-03T11:45:53+00:00 )
Feb 02, 2023 23:43 UTC
  • AI: Lazima utawala wa Israel uvunje mfumo wa ubaguzi wa rangi

Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limesema utawala wa Israel "lazima uvunje mfumo wa ubaguzi wa rangi au apathaidi ambao unasababisha mateso na umwagaji damu mkubwa" katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.

"Tangu Amnesty International ianzishe kampeni kubwa dhidi ya ubaguzi wa rangi mwaka mmoja uliopita, vikosi vya Israel vimewaua karibu Wapalestina 220, wakiwemo 35 mnamo Januari 2023 pekee," shirika hilo lilisema Jumatano katika taarifa.

"Mauaji kinyume cha sheria yaachangia kudumisha mfumo wa ubaguzi wa rangi wa Israel na hujumuisha uhalifu dhidi ya ubinadamu, kama vile ukiukwaji mwingine mkubwa na unaoendelea kufanywa na mamlaka ya Israel ikiwa ni pamoja na kuwakamata Wapalestina na kuwahamisha kwa nguvu."

Amnesty imesema kuna haja ya kuchukuliwa hatua kutokana na jinai za Israel na kutoa mfano wa tukio la tarehe 26 Januari ambapo "vikosi vya Israel vilifanya uvamizi kwenye kambi ya wakimbizi ya Jenin na kuua Wapalestina 10, akiwemo mwanamke mwenye umri wa miaka 61."

Mfano mwengine wa uchokozi wa Israel uliotajwa na taasisi ni katika kujibu mashambulizi ya Wapalestina dhidi ya walowezi wa Kizayuni katika vitongoji haramu vya Israel huko Al Quds (Jerusalem) Mashariki.

"Katika kukabiliana na shambulio hili, mamlaka za Israel zimeongeza adhabu ya pamoja dhidi ya Wapalestina, kufanya ukamataji wa watu wengi na kutishia kubomoa nyumba kama adhabu."

Ukuta wa kibaguzi uliojengwa na utawala wa kibaguzi wa Israel katika Ukingo wa Magharibi

Amnesty Internationalinasema vitendo hivyo vimefichua “mfumo wa ubaguzi wa rangi, ambapo mamlaka ya Israel inadhibiti karibu kila nyanja ya maisha ya Wapalestina na kuwaweka kwenye ukandamizaji na ubaguzi wa kila siku.”

"Wapalestina katika Maeneo Yanayokaliwa  Kwa Mabavu ya Wapalestina (OPT) wametengwa katika maeneo tofauti, huku wale wanaoishi katika Ukanda wa Gaza wakitengwa na maeneo mengine ya dunia kupitia mzingiro haramu wa Israel, ambao umesababisha mgogoro wa kibinadamu na ni aina ya adhabu ya pamoja."

Makaazi yote ya walowezi wa Israel katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na al-Quds ni kinyume cha sheria kwa mujibu wa sheria za kimataifa. Aidha, adhabu ya pamoja ni sawa na uhalifu wa kivita.