Mwakilishi wa Palestina UN: Wakati wa kukwepa adhabu Israeli umekwisha
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i94546-mwakilishi_wa_palestina_un_wakati_wa_kukwepa_adhabu_israeli_umekwisha
Balozi wa Kudumu wa Palestina katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, wakati wa Israel kukwepa adhabu umekwisha na kwamba maamuzi madhubuti na hatua za kivitendo zinapaswa kuchukuliwa ili kuuadhibu utawala huo ghasibu.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Feb 28, 2023 04:04 UTC
  • Riyad Mansour
    Riyad Mansour

Balozi wa Kudumu wa Palestina katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, wakati wa Israel kukwepa adhabu umekwisha na kwamba maamuzi madhubuti na hatua za kivitendo zinapaswa kuchukuliwa ili kuuadhibu utawala huo ghasibu.

Riyad Mansour aliyasema hayo jana katika barua tofauti kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Rais wa muda wa Baraza la Usalama na Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, akitaka kulindwa taifa la Palestina kwa mujibu wa sheria za kimataifa sambamba na kutekelezwa maazimio ya Umoja wa Mataifa kama vile Azimio 904 la Baraza la Usalama.

Azimio nambari 904 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linasisitiza ulazima wa kuungwa mkono Palestina na kupokonywa silaha walowezi wa Kizayuni katika ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu.

Huku akieleza kuwa mashambulizi ya kigaidi yanayofanywa na walowezi wa Kizayuni yamefikia kilele chake na wanaendelea kuwashambulia raia wa Palestina, Mansour ameongeza kuwa pamoja na vitendo hivyo, Wazayuni wanaharibu mali za Wapalestina katika maeneo tofauti ya Palestina na karibu na Nablus, kwa kadiri kwamba walowezi hao wamefanya mashambulizi yasiyopungua 300 katika maeneo hayo katika siku kadhaa zilizopita.

Riyad Mansour ameongeza kuwa tangu mwanzoni mwa mwaka huu, Wapalestina 65 wakiwemo watoto 13 na wazee 4 wameuawa shahidi katika hujuma za walowezi wa Kizayuni.

Mwakilishi huyo wa Palestina katika Umoja wa Mataifa amelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Baraza Kuu na nchi zote duniani, kutekeleza wajibu wao wa kimataifa wa kisheria, kiutu na kimaadili ili kuwatetea watu wasio na ulinzi wa Palestina na katika mkabala wa uvamizi na hujuma za utawala haramu wa Israel.