May 04, 2024 09:54 UTC
  • Qur'ani yavunjiwa tena heshima nchini Sweden

Mji wa Malmö nchini Sweden kwa mara nyingine umeshuhudia kkuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu. Kitendo hicho cha kuvunjia heshima Qur'ani Tukufu kimefanywa kwa ulinzi kamili wa polisi wa nchi hiyo na pia usimamizi wa jukwaa wa Wazayuni.

Shirika la Habari la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran IRNA linaripoti kwamba, mwanamke mmoja wa Sweden mwenye itikadi kali na chuki dhidi ya Uislamu jana Ijumaa alifanya kitendo cha kiovu kwa kuchoma moto nakala ya Qur'ani katika mji wa Malmö nchini Sweden.

Picha na video zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha kuwa, pamoja na mwanamke huyu ambaye ameshikilia msalaba, kuna mwanamume mmoja kando yake ambaye ameweka mabegani mwake bendera ya utawala wa Kizayuni wa Israel.

Pia, video zilizochapishwa zinaonyesha kuwa mwanamke huyo anafanya kitendo hicho kichafu cha kuchoma moto Qur'ani Tukufu akiwa na ulinzi kamili wa polisi wa Uswidi, na Waislamu pia wanatoa nara dhidi yake huku wakiwa wameshikilia bendera ya Palestina.

 

Hii si mara ya kwanza kwa serikali ya Sweden kuruhusu vitendo viovu vya kuchomwa moto nakala za Qur'ani Tukufu.

Tangu 2023, wakati Rasmus Paludan, mwanasiasa wa Denmark wa mrengo wa kulia mwenye uraia wa Uswidi, alipochoma Qur'ani mbele ya ubalozi wa Uturuki nchini Sweden, vitendo hivyo vimekuwa vikifanyika mara kwa mara nchini humo.

Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa amelaani wimbi la vitendo vya kuchomwa moto nakala za Qur'ani Tukufu katika nchi za Ulaya.