May 09, 2024 02:29 UTC
  • Bunge la Ukraine laidhinisha mpango wa kusajiliwa wafungwa jeshini

Bunge la Ukraine limepasisha muswada wa sheria inayoruhusu kukusanywa na kusajiliwa jeshini wafungwa wa nchi hiyo.

Tovuti ya habari ya Russia Today imeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, rasimu ya mwisho ya muswada huo ilipigiwa kura kwa wingi bungeni jana Jumatano baada ya kufanyiwa marekebisho ya hapa na pale.

Serikali ya Kiev ipo mbioni kusajili wanajeshi, baada ya nchi hiyo kupoteza mamia ya maelfu ya askari wake katika vita na Russia tokea mwaka 2022. 

Wiki iliyopita, Waziri wa Ulinzi wa Russia, Sergey Shoigu, alisema Ukraine imeshapoteza karibu askari wake nusu milioni tangu Februari 2022 hadi sasa, na kwamba mwaka huu pekee, nchi hiyo imepoteza wanajeshi 111,000. 

Waziri wa Ulinzi wa Ukraine, Denis Malyuska amekuwa akishinikiza kusajiliwa jeshini wafungwa hasa ambao walipatikana na hatia ya makosa ya jinai.

Wanajeshi wa Ukraine katika medani ya vita

Amewahi kusema katika mahojiano na shirika moja la habari kuwa, "(Wafungwa) ambao wamewahi kufanya mauaji huko nyuma, wanaweza kuwa wapiganaji wazuri katika medani za vita."

Kiev imeazimia kuunda vikosi maalumu vya jeshi vitakavyojumuisha wafungwa walioachiwa huru. Viongozi wa Ukraine wanasisitiza kuwa, jeshi la nchi hiyo limepata vipigo katika medani za vita kwa kutopewa msaada wa kutosha wa kijeshi na Marekani na waitifaki wake.

Tags