Marekani wanachunguza kurasa za Facebook za wasafiri
Maafisa wa idara ya uhamiaji nchini Marekani wanachunguza kursa za kijamii na hasa Facebook ya wasafiri ili kubaini misimamo yao ya kisiasa.
Kwa mujibu wa gazeti la Independent, wakili wa masuala ya uhamiaji Mana Yegani aliyeko mjini Houston, amesema wasafiri kadhaa wenye kadi ya 'Green Card' ambayo inawapa ruhusua ya kuishi na kufanya kazi Marekani, wamesimamishwa na maafisa wa uhamiaji katika viwanja wa ndege Marekani na kusailiwa kwa masaa kadhaa baada ya Rais Donald Trump kutia saini sheria ya kuwazuia raia wa nchi saba za Kiislamu kuingia nchini humo. Amesema maafisa wa usalama katika mipaka ya Marekani wanachunguza kurasa za Facebook za wasafiri kubaini mitazamo yao ya kisiasa kabla ya kuwaruhusu kuingia nchini humo.

Marufuku hiyo iliyotiwa saini na Trump inawahusu watu wenye pasipoti za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Iraq, Libya, Somalia, Sudan, Syria na Yemen. Hata raia wa nchi hizo walio na 'Green Card' pia wamepigwa marufuku kuingia Marekani.
Hatua hiyo ya kibaguzi ya Trump imeendelea kulaaniwa na kukosolewa katika kila kona ya dunia.