Waitifaki wa Marekani wapunguza nusu ya askari wao nchini Iraq
Nchi 29 wanachama wa muungano wa kijeshi unaoongozwa na Marekani nchini Iraq zimepunguza kwa asilimia 50 idadi ya wanajeshi wao vamizi katika nchi hiyo ya Kiarabu.
Hayo yaliripotiwa jana Jumatano na gazeti la New York Times la Marekani ambalo limeeleza kuwa, muungano huo vamizi wa kijeshi umepunguza wanajeshi 1,200 kutoka Iraq.
Ripoti zinasema kuwa, muungano huo umedai kuwa umechukua hatua hiyo kutokana na janga la corona lililoua malaki kote duniani.
Kuna wanajeshi 5,200 wa Marekani nchini Iraq, lakini Wizara ya Ulinzi ya nchi hiyo (Pentagon) inakabiliwa na mashinikizo makubwa ya kutakiwa ivondoe vikisi vyake vyote au ipunguze idadi ya askari hao kutoka nchi hiyo ya Kiarabu.
Hii ni katika hali ambayo, Januari 5 mwaka huu, Bunge la Iraq lilipiga kura na kupitisha mpango uliopendekezwa na wabunge wa kuhitimisha makubaliano ya kijeshi yaliyofikiwa kati ya nchi hiyo na Marekani na kuwataka wanajeshi wa Marekani waondoke nchini humo.
Kikao hicho cha dharura cha Bunge la Iraq kilifanyika baada ya vikosi vamizi vya US kutumia ardhi ya nchi hiyo ya Kiarabu kutekeleza mauaji ya kigaidi dhidi ya Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, Shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani na naibu mkuu wa jeshi la kujitolea la wananchi wa Iraq la al-Hashdu as-Sha'abi.