WHO: Chanjo ya China ni salama
Shirika la Afya Duniani WHO limesema kuwa chanjo za corona zilizotengenezwa China ni za kuaminika na wala hazina hatari yoyote.
Akizungumza katika kikao maalumu kilichofanyika jana Jumatano kuhusu corona, Alejandro Cravioto Mkuu wa Ujumbe wa Ushauri wa Shirika la Afya Duniani alisema kuwa chanjo za Sinovac na Sinopharm zimekuwa na taathira na matokeo mazuri katika kukabiliana na virusi vya corona, matokeo ambayo ni ya kiwango cha juu katika uwanja huo na kwamba yanayokwenda sambamba na viwango vinavyohitajika na WHO.
Cravioto ambaye ni mtaalamu wa ushauri wa kistratijia wa Shirika la Afya Duniani (SAGE) anatumai kwamba kundi lake litaweza kutoa ushauri muhimu na wa dharura kuhusiana na chanjo hizo kufikia mwishoni mwa mwezi huu wa Aprili. Amesisitiza kwamba matumizi ya chanjo hizo bila shaka yanahitajia usimamizi wa karibu wa WHO.
Margaret Harris, Msemaji wa Shirika la Afya Duniani alisema mwanzoni mwa mwezi uliopita wa Machi kwamba chanjo mbili hizo za China zingepewa kipaumbele katika orodha ya dharura ya shirika hilo kwa manufaa ya wanadamu.