Sep 21, 2023 02:26 UTC
  • Alkhamisi, tarehe 21 Septemba 2023

Leo ni Alkhamisi tarehe 5 Mfunguo Sita Rabiul Awwal 1445 Hijria inayosadifiana na tarehe 21 Septemba 2023.

Siku kama ya leo miaka 191 iliyopita, inayosadifiana na 21 Septemba 1832, aliaga dunia Sir Walter Scott, mwandishi wa riwaya, mshairi na mwanahistoria mahiri wa Uskochi. Alizaliwa 15 Agosti mwaka 1771 na baada ya kuhitimu masomo yake katika taaluma ya sheria, alifanya kazi ya uwakili kwa muda wa miaka 14. Hata hivyo, Sir Scott alikuwa na shauku na mapenzi makubwa na taaluma ya fasihi ya lugha.

Walter Scott

Siku kama ya leo miaka 114 iliyopita, yaani 21 Septemba 1909, alizaliwa Dakta Osagyefo Kwame Nkrumah mwanasiasa na shujaa wa uhuru wa Ghana.

Nkrumah alishiriki kikamilifu katika harakati za kupigania uhuru za wananchi wa Ghana dhidi ya mkoloni Muingereza. Baada ya kujipatia uhuru, kulijitokeza na kushuhudiwa njama kadhaa za kutaka kumuondoa madarakani na hata kumuua Nkrumah. Mwaka 1966 wakati Dakta Nkrumah akiwa safarini nchini China, Jenerali Joseph Ankrah alifanya mapinduzi na kuiondoa madarakani serikali Nkrumah. Mwanamapinduzi huyo aliaga dunia mwaka 1972 akiwa uhamishoni nchini Romania.

Kwame Nkrumah alikuwa na nafasi muhimu katika kuasisiwa Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Siasa za Upande Wowote NAM pamoja Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika OAU.

Katika siku kama ya leo miaka 29 iliyopita Bunge la Taifa la Ufaransa lilipasisha sheria iliyopiga marufuku vazi la staha la mwanamke wa Kiislamu, hijabu katika shule za nchi hiyo.

Ufaransa ilipasisha sheria hiyo inayowazuia wanafunzi wa kike Waislamu kwenda mashuleni wakiwa na vazi la hijabu licha ya kudai kuwa ni kitovu cha demokrasia na uhuru. Baadaye sheria hiyo ilipanuliwa zaidi na kupiga marufuku vazi la hijabu katika vyuo vikuu na idara za umma. Wachambuzi wengi walikosoa vikali sheria hiyo wakisema inapingana na Katiba ya Ufaransa na Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu zinazosisitiza kuwa kila mtu ana uhuru wa kukubali na kutekeleza itikadi zake za kidini maadamu hazina madhara kwa watu wengine. 

Na leo Septemba 21 ni Siku ya Alzheimer's Duniani.

Ugonjwa wa Alzheimer's hutokana na tatizo la neva na husababisha kufa taratibu kwa seli za ubongo na kuzuia matatizo ya kumbukumbu, kufikiri na katika mienendo ya mgonjwa. Pia, ugonjwa huu ndiyo sababu maarufu zaidi ya tatizo la akili la ugonjwa wa kupoteza fahamu, dementia.

Kulingana na ripoti ya hivi karibuni ya Shirika la Afya Duniani (WHO), mtu mmoja ulimwenguni hugunduliwa na ugonjwa wa Alzheimer kila sekunde 68. Hivi sasa, zaidi ya watu milioni 50 duniani wanasumbuliwa na ugonjwa wa Alzheimer, na inatabiriwa kuwa idadi ya watu wenye tatizo la akili la dementia itafikia milioni 82 ifikapo 2030, na milioni 152 ifikapo 2050.

Siku ya Alzheimer Duniani ni kampeni ya kimataifa ambayo hufanyika kila mwezi Septemba ili kuongeza ufahamu na kupinga unyanyapaa wa watu wenye tatizo hilo la akili.

Kauli mbiu na mada ya kampeni ya Siku ya Alzheimer Duniani ya 2023 ni: "Never too early never too late" (Kamwe si mapema sana wala hujachelewe sana). Lengo la kaulimbiu hiyo ni kusisitiza jukumu kuu la kutambua sababu za hatari ya tatizo hilo na kuchukua hatua haraka za kuzuia hatari hiyo.

 

Tags