Uislamu Chaguo Langu (97)
Hamjambo wapenzi wasikilizaji na karibuni kujiunga nami katika kipindi hiki ambacho huwaangazia watu ambao baada ya kufanya utafiti wa kina huamua kufuata njia iliyojaa nuru maishani yaani Uislamu. Katika makala yetu ya leo tutamuangazia mwanamke Mmarekani aliyesilimu. Karibu kujiunga nami hadi mwisho.
Twahira ni mwanamke Mmarekani aliyesilimu na ambaye sasa ni mama mzazi
wa mtoto wa kiume aliyepewa jina la Hafidh na mtoto wa kike aliyepewa
jina la Sabira.
Bi. Twahira alizaliwa katika jimbo la New York na
aliikubali dini tukufu ya Kiislamu mwaka 2007. Mwaka mmoja baada ya
kusilimu alipata taufiki ya kuwa mfuasi wa madhab ya Shia Ithnaashari.
Bi. Twahira alizaliwa katika familia ya Kikristo na kutokana na kuwa
mfanyakazi wa Wizara ya Afya ya Marekani alipata fursa ya kusafiri
katika maeneo mbali mbali ya dunia.
Bi. Twahira anabainisha
alivyopata taufiki ya kusilimu ifuatavyo: "Katika mwaka wa mwisho wa
masomo ya shule ya sekondari nchini Marekani huwa kuna somo la
kuarifisha dini muhimu zaidi duniani. Nakumbuka tukifundishwa kuhusu
misingi ya dini ya Kiislamu na kwa mujibu wa tuliyoyasoma dini hii
ilikuwa ngumu sana kuifuata. Wakati huo nilikuwa Mkristo aliyekuwa na
imani thabiti na baba yangu alinifunza misingi yote ya Ukristo. Mwaka
2007 nilifunga safari na kuelekea Afrika. Ilikuwa ni katika Mwezi
Mtukufu wa Ramadhani na nilihudumu kama mfanyakazi wa afya katika nchi
za Kiislamu za Somalia, Djibouti na nchi ya Eritrea yenye idadi kubwa ya
Waislamu. Kitu ambacho kilinishangaza ni kuwa, licha ya Waislamu wa
nchi hizo kuwa ni watu masikini na wenye maisha magumu lakini
walifungamana kikamilifu na mafundisho ya Uislamu. Hali ya hewa katika
nchi hizo ni ya joto la juu sana lakini Waislamu walikuwa wakifunga
kikamilifu kula na kunywa katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani huku
wakitekeleza ibada nyinginezo kama vile kuswali. Suala hili la
kufungamana Waislamu na mafundisho ya dini yao katika hali ngumu kama
hiyo ni jambo ambalo lilinipelekea nifanye utafiti zaidi kuhusu
Uislamu."
Mwanamke huyu Mmarekani aliyesilimu anaendelea kusema:
"Baada ya kuvutiwa na namna Waislamu wanavyofungamana na dini yao,
niliporejea Marekani nilianza kusoma vitabu vya Kiingereza kuhusu
Uislamu. Katika kipindi hicho niliweza kujuana na Mwislamu ambaye
aliweza kunifunza mengi zaidi kuhusu mafundisho ya Uislamu. Kwa hakika
nilivutiwa sana na mafundisho ya dini tukufu ya Kiislamu na niliweza
kupata majibu ya maswali mengi ambayo nilikuwa nayo. Nilianza kuenda
katika msikiti na kujifunza lugha ya Kiarabu ili niweze kuisoma Qur'ani
Tukufu kwa lugha yake asili yaani Kiarabu. Utafiti na uchunguzi wangu
ulinivuta zaidi katika Uislamu. Hatua kwa hatua nilianza kufahamu kuwa
Uislamu ndiyo dini bora na kamili zaidi ya Mwenyezi Mungu. Kwa msingi
huo niliamua kusilimu," anasema Bi. Twahira.
@@@
Baada ya kusilimu
Bi Twahira alijitahidi sana kutekeleza mafundisho ya Kiislamu na
alifanikiwa katika hatua alizozichukua. Hapa anafafanua zaidi kwa
kusema: "Nilianza kuandika mafundisho ya Kiislamu na nilijitahidi
kuyatekeleza katika maisha yangu. Katika sehemu niliyokuwa nikifanya
kazi wengi walistaajabu kuona nikitekeleza ibada za Kiislamu. Wakati wa
kuswali nilikuwa nikitumia chombo maalumu kutafuta qibla. Kwa muda mrefu
mkurugenzi wangu hakuwa amefahamu kuwa mini ni Mwislamu na kwamba
nilikuwa nikiswali kazini. Baadaye ilimbainikia kuwa mimi, mwanamke
Mmarkenai Mzungu, nimesilimu jambo ambalo lilimshangaza sana. Alikuwa na
dhana potofu kuwa Uislamu ni dini ambayo wanaume wanaoifuata huwapiga
ovyo wanawake na hivyo alipinga ibada niliyokuwa nikifanya. Kwa bahati
nzuri mkurengezi huyo aliondolewa na mahala pake akaja mtu mwenye
mantiki ambaye aliweza kunidiriki na hivyo aliniruhusu kufanya ibada
katika wakati maalumu. Kwa muda mrefu baada ya kusilimu sikuwa nikivaa
hijabu kwani hali yangu ya kikazi haikuniruhusu kufanya hivyo. Fauka ya
hayo nguo tulizokuwa tukivaa zilikuwa ni za mikono mifupi. Lakini baada
ya kupata maelezo kamili kuhusu umuhimu na ulazima wa kuvaa Hijabu,
nilianza kuvaa vazi hilo la stara," anasema Mmarekani aliyesilimu, Bi.
Twahira.
Kwa mtazamo wa wanafikra na wanazuoni, adhama ya dini ambayo
risala yake ililetwa na Mtume Mohammad SAW ni nukta mbili. Awali ni
Qur'ani Tukufu ambayo ni burhani inayosomwa kwa lugha yake asili. Pili
ni shakhsia kubwa na ya kipekee ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mohamad Al
Mustafa SAW. Kwa hakika mtukufu huyo ni nyota ya kipekee inayoangaza
dunia. Ni nyota ambayo inaendelea kuleta nuru na karama kila mahala.
Moja ya sifa za kipekee za Mtume Mtukufu wa Uislamu ni elimu inayoenda
sambamba na maadili, hekima, uafilifu na heshima. Hivi sasa baada ya
kupita zaidi ya miaka 1,400 tokea alipozaliwa, Mtume Muhammad SAW
anaendelea kuvutia idadi kubwa ya wanaadamu. Mmarekani aliyesilimu Bi.
Twahira anabainisha mtazamo wake kuhusu baadhi ya sifa za kipekee za
Mtukufu Mtume kwa kusema: "Mtume Muhammad SAW alikuwa shakhsia mwenye
malengo ya juu na ya kipekee. Ameweza kutoa masomo yenye thamani za juu
kwa wanaadamu. Uhusiano wa Mtume wa Uislamu na Mayahudi wa zama zake ni
jambo ambalo liliniathiri sana. Nukta nyingine iliyonivutia katika
shakhsia ya Mtume Mtukufu ni ibada yake katika pango la Hiraa."
Mmarekani
aliyesilimu Bi. Twahira anaongeza kuwa nukta nyingine iliyompelekekea
asilimu ni utamaduni tajiri wa kifikra katika Uislamu. Anasema Waislamu
wana umaanawi wa kina ambao hauko tena katika nchi za Magharibi. Bi.
Twahira anasema baada ya kusilimu aliolewa na Mwisllamu na hapo akaweza
kuujua zaidi Uislamu. Anaongeza kuwa hatua kwa hatua alipata taufiki ya
kuujua utamaduni wenye thamani wa Ahul Bayt wa Mtume SAW ambao amewataja
kuwa kigezo cha maisha bora na sahihi ya Kiislamu. Mmarekani huyu
aliyesilimu ambaye sasa anafuata madhehebu ya Shia Ithnaashari anasema:
"Ningali ninakumbuka vizuri majlisi ya kuomboleza kuuawa shahidi Imam
Hussein AS. Nilikuwa sijawahi kupata tajriba kama hiyo. Baada ya
kuchunguza maisha ya Ahul Bayt wa Mtume SAW niliweza kuufahamu Uislamu
kikamilifu". Anaelezea zaidi kuhusu namna alivyoyakubali madhehebu ya
Shia Ithnaashari kwa kusema: "Ushia ulinivutia sana kutokana na
utamaduni wake wa kujitolea muhanga. Kwa hakika utamaduni wa kufa
shahidi ni mkabala ya kujipenda." Mmarekani huyu aliyesilimu anasema
katika kuimarisha maarifa yake alisoma kitabu kilichoandikwa na
Ayatullah Sistani chenye anwani ya "Sheria za Kiislamu". Aidha alisoma
kitabu cha Imam Ghazali chenye anwani ya "Kuhuisha Sayansi za Dini" au
Ihya Ulumu Din, kitabu cha Ayatullah Amini kuhusu 'Mwanaadamu Kujijenga
Nafsi' na kitabu maarufu cha Sheikh Mufid chenye anwani ya Al Irshad au
Muongozo.
Mmarekani huyo aliyesilimu pia amevutiwa sana na malenga na
wanafasihi Waislamu. Anaongeza kuwa: "Kabla ya kusilimu nilisoma athari
za malenga Wairani Waislamu kama vile Maulana, Attar, Hafidh na Saadi.
Umaridadi wa Irfani katika mashairi ya Kifarsi ni nukta iliyonivutia
katika Uislamu." Anasema mvuto wa mashairi ya lugha ya Kifarsi ni moja
ya sababu zilizompelekea ampe mtoto wake jina la Hafidh, ambaye alikuwa
malenga maarufu Muirani.