Chad yakanusha taarifa kuhusu kurejeshwa askari wa Marekani nchini humo
Waziri wa Mambo ya Nje wa Chad Abderaman Koulamallah amekanusha madai ya Jenerali wa Marekani Kenneth Eckman wa Kamandi ya Kijeshi ya Marekani Afrika (AFRICOM) kuhusu kurejea wanajeshi wa Marekani nchini mwake, kwa madai kuwa ni kwa ombi la N'Djamena.
Koulamallah amesema katika taarifa yake kwamba, "Hakujakuwa na mawasiliano na idara za kijeshi za Marekani na tunakanusha kabisa habari hii. Hatujajadiliana na serikali ya Marekani kuhusu kurejea kwa wanajeshi wake nchini Chad."
Ameongozea kuwa Chad ni nchi huru na itasalia kuwa msimamizi wa maamuzi yake kuhusu usalama wa taifa na ushirikiano wa kijeshi na washirika wake wa kimataifa.
Katika mahojiano na Sputnik, Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani wa Chad Ibrahim al Asil amesema kuwa maoni ya wananchi nchini humo ni dhidi ya uwepo wa jeshi la Ufaransa na Marekani na kwamba wanajeshi wa Marekani hawataruhusiwa kurudi tena nchini humo.