Ghasia za kisiasa zapamba moto DRC
Mivutano ya kisiasa imeripotiwa kupamba moto nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Maandamano ya wapinzani huko Kongo yamesababisha mapigano makali kati ya polisi na waandamanaji; ambapo wafanya maandamano walichoma moto ofisi za serikali katika mitaa ya mji mkuu Kinshasa. Pamoja na viongozi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kupiga marufuku maandamano ya wapinzani kote nchini humo, lakini ghasia zinaendelea kushuhudiwa katika mitaa mbalimbali ya nchi hiyo huku polisi wakifanya kila wawezalo kutuliza ghasia na kudumisha amani. Mivutano ya kisiasa Kongo inaongezeka kila uchao huku weledi wa mambo katika eneo wakitaja kuendelea hatua za serikali ya nchi hiyo za kuchelewesha uchaguzi na kudhibiti Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwa ni sababu inayoshadidisha hali ya mchafukoge na ukosefu wa amani huko Kongo. Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Kongo hivi karibuni alitangaza kuwa uchaguzi wa rais utafanyika mwezi Disemba mwaka 2018.