Waasi wa Maï-Maï watakiwa kuweka chini silaha DRC
Jumuiya za kiraia katika mkoa wa Kivu Kaskazini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, zimewataka waasi wa Maï-Maï kuweka chini silaha zao.
Jumuiya hizo za kiraia zimelitaka jeshi la nchi hiyo kwa kushirikiana na askari wa kusimamia amani wa Umoja wa Mataifa kuendesha operesheni kubwa kwa lengo la kuwanyang'anya silaha waasi hao wanaoendesha harakati zao katika maeneo ya Rutshuru na Lubero kwenye mkoa wa Kivu Kaskazini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Kadhalika jumuiya hizo zimeonyesha wasi wasi wake juu ya kuzuka mgogoro baina ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Uganda, kufuatia mashambulizi ya waasi hao wa Maï-Maï.
Mbali na hayo, jumuiya hizo za kiraia zimewatuhumu viongozi wa waasi hao kwa kupora mali za raia wa nchi hiyo. Ndjike Kaiko, msemaji wa moja ya jumuiya hizo amenukuliwa akielezea, kuwepo mipango ya kuanzishwa operesheni kabambe dhidi ya waasi hao. Itafaa kuashiria kuwa, maeneo ya mashariki na kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yamekuwa yakishuhudia machafuko kwa kipindi cha miaka 20 sasa, huku udhaifu wa jeshi la serikali na askari wa kofia ya buluu wa Umoja wa Mataifa, vikitajwa kuwa sababu kuu ya kadhia hiyo.