ICC yamuongeza Bemba mwaka mmoja jela kwa kuwahonga mashahidi
Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC imemhukumu mwaka mmoja jela, Makamu wa Rais wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Jean-Pierre Bemba, baada ya kupatikana na hatia ya kuwapa rushwa mashahidi katika kesi kuu ya awali dhidi yake.
Jaji Mkuu katika kesi hiyo Bertram Schmitt amesema hukumu hiyo ya miezi kumi na miwili jela itaandamana na hukumu ya awali ya miaka 18 jela, iliyotolewa na mahakama hiyo ya mjini The Hague nchini Uholanzi. Kadhalika Jaji Bertram Schmitt amemuagiza Jean-Pierre Bemba alipe faini ya Dola 323 640 za Marekani.
Wapambe wanne wa Bemba, wakiwemo mawakili na mashahidi wanaofahamika kama Aime Kilolo, Jean-Jacques Mangenda, Narcisse Arido, na Fidele Babala wamehukumiwa na ICC vifungo vya kati ya miezi sita na miaka miwili na nusu jela kwa kushirikiana na Makamu huyo wa Rais wa zamani wa Kongo DR.
Juni mwaka jana 2016, mahakama ya ICC ilimhukumu miaka 18 jela Bemba, baada ya kupatikana na hatia ya kutenda jinai za kivita katika nchi jirani ya Jamhuri ya Afrika ya Kati kati ya mwaka 2002-2003.
Jaji Sylvia Steiner alifafanua kuwa, ICC imemhukumu Bemba kifungo cha miaka 18 jela, kwa kupatikana na hatia ya kutenda jinai za kivita na ubakaji dhidi ya binadamu, kwa kuwatuma wapiganaji wa MLC katika Jamhuri ya Afrika ya Kati mwaka 2003 ili kusaidia kuzima mapinduzi ya kijeshi dhidi ya rais wa wakati huo, Ange -Felix Patasse.
Hukumu dhidi ya Bemba ilikuwa ya kwanza dhidi ya Makamu wa Rais wa zamani katika mahakama hiyo ya kimataifa iliyobuniwa mwaka 2002, ili kukabiliana na makosa ya jinai na haswa ya kivita.