UN yalaani shambulizi dhidi ya askari wa kusimamia amani huko Sudan Kusini
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, limelaani shambulizi la hivi karibuni la waasi wa Sudan Kusini dhidi ya askari wa kusimamia amani wa umoja huo katika mji wa Leer, magharibi mwa mkoa wa Upper Nile.
Baraza hilo sambamba na kulaani hujuma hiyo, limevitaka vyama vya siasa na waasi wa Sudan Kusini kuhitimisha ukatili na kufungamana na hati ya Baraza la Usalama la UN kwa ajili ya kuhitimisha mapigano nchini.
Itakumbukwa kuwa, Jumatano iliyopita, waasi wa Sudan Kusini walishambulia msafara wa askari wa kusimamia amani wa Umoja wa Mataifa, ambao akthari yao walikuwa na uraia wa Ghana. Kabla ya hapo kamisheni ya waangalizi ya Umoja wa Mataifa ilitangaza kuwa, ushahidi unaonyesha kuwa, serikali ya Juba imejikita katika kununua silaha kwa ajili ya jeshi, vyombo vya usalama na makundi ya wanamgambo washirika wake.
Sudan Kusini ilitumbukia katika machafuko mwaka 2013 baada ya Rais Salva Kiir kumtuhumu aliyekuwa makamu wake Riek Machar kwamba alipanga njama ya kutaka kumuondoa madarakani. Katika machafuko hayo maelfu ya watu wameuawa na zaidi ya wengine milioni moja kuwa wakimbizi katika nchi jirani.