Rwanda yamshtaki mkosoaji wa Rais kwa kuchochea uasi
Msemaji wa Mwendesha Mashtaka wa serikali ya Rwanda amesema leo kuwa, mamlaka husika za Rwanda zimemfungulia mashtaka mkosoaji wa Rais Paul Kagame kwa kosa la kuchochea uasi na kughushi baada ya kuzuiwa kuchuana na hasimu wake Kagame katika uchaguzi wa rais wa mwezi Agosti mwaka huu.
Diane Shima Rwigara aliye na umri wa miaka 35 ambaye ni mhasibu kitaaluma amekuwa akimtuhumu Rais Kagame kwa kuwabinya wapinzani na kukikosoa chama tawala cha RPF kwa kuweko madarakani tangu kiliposhika hatamu za uongozi na kuhitimisha mauaji ya kimbari nchini humo mwaka 1994. Kagame alishinda uchaguzi huo wa rais kwa kupata asilimia 98.8 ya kura.
Mama yake Diane Rwigara, Bi Adeline na dada yake aliyetajwa kwa jina la Anne pia wameshtaki kwa uchochezi, ubaguzi na udini. Hayo yameelezwa na Mwendesha Mashtaka Faustin Nkusi. Wanawake hao watatu wamekuwa korokoroni kwa wiki zipatazo mbili. Tarehe 30 mwezi Agosti watuhumiwa hao walichukuliwa nyumbani kwao Kigali kwa madai ya kudaiwa kukwepa kulipa kodi zinazoihusu kampuni ya tumbaku inayomilikiwa na familia hiyo. Hata hivyo tuhuma hii ya kukwepa kulipa kodi haijajumuishwa katika tuhuma zilizosomwa jana dhidi yao.