Boko Haram yaua raia 10 katika shambulizi la kigaidi nchini Nigeria
Habari kutoka Nigeria zimeripoti kwamba kwa akali raia 10 wameuawa na wanamgambo wa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Boko Haram katika mashambulizi matatu tofauti, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Taarifa iliyotolewa na kundi moja la wanamgambo linaloshirikiana na serikali ya Nigeria imesema kuwa, watu saba wameuawa katika eneo la Dikwa, wilaya ya Gamboru jimbo la Borno, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika. Kwa mujibu wa taarifa hiyo raia watatu wengine waliuawa katika hujuma nyingine eneo la Kasuwar Shanu na Fulatari katika jimbo hilo hilo la Borno. Kundi hilo jipya la wanamgambo limekuwa likishirikiana na jeshi la serikali ya Abuja katika vita vyake dhidi ya wanachama wa kundi la Boko Haram.
Licha ya serikali ya Nigeria kushirikiana na nchi za eneo la Ziwa Chad kuendesha operesheni kali dhidi ya kundi la Boko Haram, lakini hadi sasa kundi hilo limeendelea kutekeleza mashambulizi katika maeneo tofauti ya Nigeria na nje ya nchi hiyo. Inaelezwa kuwa, udhaifu wa serikali ya Abuja katika kukabiliana na genge hilo la Kiwahabi, ni sababu ya kuendelea mashambnulizi ya kila uchao ya wanachama wa kundi hilo.