UNHCR: Misaada itolewe kwa ajili ya kuimarisha amani Libya, Mali na Niger
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i46348-unhcr_misaada_itolewe_kwa_ajili_ya_kuimarisha_amani_libya_mali_na_niger
Mkuu wa Kamisheni Kuu ya Wakimbizi ya Umoja wa Mataifa ametoa wito wa kutolewa misaada ya kifedha kwa ajili ya kuimarisha amani katika nchi za Mali, Niger na Libya.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 26, 2018 10:11 UTC
  • UNHCR: Misaada itolewe kwa ajili ya kuimarisha amani Libya, Mali na Niger

Mkuu wa Kamisheni Kuu ya Wakimbizi ya Umoja wa Mataifa ametoa wito wa kutolewa misaada ya kifedha kwa ajili ya kuimarisha amani katika nchi za Mali, Niger na Libya.

Filippo Grandi aliyekuwa safarini katika nchi za Libya, Niger na Mali amezitaka nchi wafadhili kuchukua hatua za kuimarisha amani na usalama katika nchi hizo kwa sababu raia wao wengi wanakimbilia Ulaya kutokana na ukosefu wa amani katika nchi zao.

Mkuu wa Kamisheni Kuu ya Wakimbizi ya UN amesema kuwa, jamii, wakimbizi na wahajiri walioko katika nchi hizo wanahitajia amani na utulivu lakini rasilimali zilizopo ni ndogo sana. 

Filippo Grandi akiwa pamoja na wakimbizi, Mali

Filippo Grandi ameongeza kuwa, watu wa Ulaya wamekuwa wakilalamika kuhusu wahajiri na wakimbizi wanaoingia katika nchi zao kinyume cha sheria lakini wanapaswa kuelekea kwamba hali itaendelea kuwa hivyo hadi pale kutakapofanyika uwekezaji halisi barani Afrika.

Katika miezi kadhaa ya hivi karibuni wakimbizi karibu elfu tano wa Burkina Faso wameingia nchini Mali wakikimbia vita na mapigano yanayoendelea maeneo ya mpakani kati ya jeshi la nchi yao na makundi ya waasi.